TANESCO WAZUA BALAA LA MAJI SHINYANGA KUKATA UMEME KASHWASA...WANANCHI WALIA NA SERIKALI


Wakazi wa mkoa wa Shinyanga wameitaka serikali kuchukua hatua za haraka ili waendelee kupata huduma ya maji safi na salama baada ya kukosa maji kwa kipindi cha siku saba tangu Januari 18 mwaka huu. 

Wananchi wa Mji wa Shinyanga na Kahama wamekumbwa na adha ya kukosa huduma ya maji baada ya Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Kahama Shinyanga (KASHWASA) kukatiwa umeme na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO). 

TANESCO wamekata umeme katika chanzo kikuu cha maji ya Ziwa Victoria kilichopo Ihelele wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza ambacho ni tegemeo kubwa la wakazi wa mkoa Shinyanga na mikoa ya jirani. 

Wananchi wamekosa huduma ya maji tangu kutolewa tangazo na SHUWASA na KUWASA kwamba kutakuwa na upungufu wa maji kutokana na KASHWASA inayowauzia maji kukatiwa umeme,tatizo ambalo linatokea zikiwa ni siku nne tu kupita baada ya Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso kumaliza ziara yake mkoani Shinyanga Januari 13,2018 na kuahidi kushughulikia tatizo hilo wizarani. 

Wakizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti wakazi wa mji wa Shinyanga na Kahama wamesema kukosekana kwa huduma ya maji kunahatarisha afya zao kwani wanaweza kukumbwa na mlipuko wa magonjwa kutokana na kutumia maji yaliyotuama kwenye madimbwi na majaruba ambayo siyo salama. 

Mbali na afya zao kuwa hatarini,pia wananchi wanatumia gharama kubwa kununua maji.

Mwenyekiti wa bodi ya Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mji wa Kahama (KUWASA) Bahati Matala hivi karibuni wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Maji wilayani Kahama,alisema changamoto kubwa inayowakabili ni wananchi kukosa huduma ya maji linapotokea tatizo la KASHWASA kukatiwa umeme wakati KUWASA haidaiwi na KASHWASA inayowauzia maji na kuitaka serikali kulifanyia kazi suala hilo. 

Akitoa taarifa kwa Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso ,Mkurugenzi wa (KASHWASA) Joshua Mgeyekwa alisema changamoto iliyopo ni deni kubwa la umeme la kuendesha mitambo ya kuzalisha maji, ambapo hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Desemba 2017 deni lilikuwa limefikia shilingi bilioni 2.265 ambalo limesababishwa kwa kiasi kikubwa na serikali kwa kutolipa sehemu yake ya gharama za umeme ambayo ni 20%. 

Mgeyekwa alisema mbali na deni la serikali pia Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA) hadi kufikia Januari 11, 2018 wakati wakitoa taarifa kwa Naibu Waziri wa Maji,walikuwa wanadaiwa shilingi bilioni 1.079 ,huku mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira Ngudu,Mwanza(NGUWASA)ikidaiwa shilingi milioni 88 na KUWASA haidaiwi.

Januari 18,2018 Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira mjini Shinyanga (SHUWASA) na Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira mjini Kahama (KUWASA) zilizitoa matangazo kuwataarifu wateja wao kuhusu upungufu wa maji..soma hapa chini

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527