HATIMAYE MTOTO SALAWA MIHANGWA AFANYIWA UPASUAJI WA MOYO JKCI KWA MSAADA WA MBUNGE AZZA HILAL




Mtoto Salawa Mihangwa (kushoto) akiwa na mama yake baada ya kufanyiwa upasuaji katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es salaam


Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) imefanikiwa kumfanyia upasuaji mtoto mtoto Salawa Mihangwa (03) mkazi wa kijiji cha Solwa kata ya Solwa wilaya ya Shinyanga mkoani Shinyanga aliyekuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa moyo.

Mtoto huyo alifikishwa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es salaam na Mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Shinyanga,mheshimiwa Azza Hilal Hamad (CCM) aliyeguswa na ugonjwa wa moyo huku mzazi wa mtoto huyo akiwa hana uwezo wa kifedha kufanikisha upasuaji huo na kuamua kumchukua mtoto huyo kutoka kijijini kwao.

Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi na daktari bingwa wa magonjwa ya moyo Profesa Mohamed Janabi amesema mtoto huyo amefanyiwa upasuaji hivi karibuni na ameruhusiwa kurudi nyumbani na hali yake inaendelea vizuri.

“Mtoto aliletwa na mheshimiwa Azza Hilal,tumemfanyia upasuaji wa kutumia njia ya kisasa ya kupasua kifua na kuziba tundu na kurekebisha mifupa yake ya damu ambayo haikukaa sawa”,alisema Prof . Janabi.

“Uzuri wa hii Oparesheni ya kutopasua kifua ni kwamba wiki hiyo hiyo tunayomfanyia upasuaji tunamruhusu kurudi nyumbani na anaendelea vizuri”,aliongeza.

Naye mbunge aliyesaidia kufanikisha matibabu kwa mtoto huyo,Mheshimiwa Azza Hilal amesema baada ya kuguswa na hali aliyokuwa nayo mtoto huyo aliamua kuchukua vyeti vya mtoto na kumkatia bima ya na kumsafirisha kutoka kijijini hadi jijini Dar es salaam.

Mbunge aliishukuru serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuendelea kuwapatia matibabu wagonjwa hususani ambao hawana uwezo huku akiwaasa wazazi kukata bima za afya bima kusaidia katika huduma za matibabu kwani matibabu bila kuwa na bima ya afya ni gharama kubwa. 

“Namshukuru mwenyezi mungu kwa wema wake ulio mkuu,mtoto huyu nilikutana naye katika kijiji cha Solwa kwenye zahanati ya Solwa akiwa na tatizo la moyo ambapo mama yake ambaye ni ibint aliyepewa Ujauzito baada ya kumaliza darasa la saba,mtoto alizaliwa na tatizo la moyo na mzazi alikosa fedha kwa ajili ya upasuaji”,alieleza Mbunge huyo.

“Kutokana na kuguswa na hali aliyokuwa nayo mtoto huyo nilichukua vyeti vyake nikaenda navyo jijini Dar es salaam Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) na tayari amefanyiwa upasuaji nilijitolea kumkatia Bima ya afya ya watoto yenye gharama ya shilingi 50400/= inayomuwezesha kupatiwa matibabu katika hospitali yoyote hapa nchini”,aliongeza.

Tarehe 11.05.2017 akiwa katika ziara kwenye zahanati ya Solwa iliyopo katika kijiji cha Solwa,kata ya Solwa,jimbo la Solwa mkoa wa Shinyanga,Mheshimiwa Azza Hilal baada ya kukutana na mtoto huyo aliahidi kutafuta namna ya kumsaidia.

Mtoto huyo alikuwa akilelewa na kupatiwa huduma za kiafya katika zahanati ya Solwa baada ya mzazi wake kukosa pesa kwa ajili ya mtoto huyo kufanyiwa upasuaji.
Mei 11,2017-Mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Shinyanga,mheshimiwa Azza Hilal Hamad (CCM) akiwa amembeba mtoto Salawa Mihangwa (03) aliyekuwa ana tatizo la ugonjwa wa moyo akisikiliza maelezo ya mzazi wa mtoto huyo Grace Richard (kushoto) aliyekosa pesa kwa ajili ya mtoto huyo kufanyiwa upasuaji.
Mei 11,2017- Mganga Mfawidhi wa zahanati ya Solwa Dkt. Edwin Ibrahim akimwonesha mheshimiwa Azza Hilal Hamad vyeti vya mtoto Salawa Mihangwa aliyekuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa moyo na alikuwa akilelewa katika zahanati ya Solwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527