Picha : RPC SIMON HAULE AFUNGA MAADHIMISHO YA WIKI YA NENDA KWA USALAMA BARABARANI MKOA WA SHINYANGA MWAKA 2017

Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule amefunga wiki ya nenda kwa usalama barabarani mkoa wa Shinyanga yaliyoanza siku ya Jumatatu Novemba 13,2017 katika viwanja vya jeshi la Zimamoto mjini Shinyanga.


Akizungumza leo Jumamosi Novemba 18,2017 wakati wa kufunga maadhimisho hayo, yenye kauli mbiu "Zuia ajali,Tii sheria,Okoa Maisha",Kamanda Haule aliwataka watumiaji wa barabara kuzingatia alama na michoro ya barabarani na watembea kwa miguu kuhakikisha wanapokuwa barabarani wanavuka katika maeneo yanayostahili ili kupunguza ajali zisizo za lazima.



“Watembea kwa miguu hakikisheni mnavuka katika maeneo yanayotakiwa,ajali nyingi zinatokea kutokana na uzembe wa watumiaji wa barabara,na ajali zinazoongoza Shinyanga ni za pikipiki na watembea kwa miguu”,alisema.


Katika hatua nyingine aliwataka wananchi kulinda miundombinu ya barabara kwa kushirikiana na serikali na kuhakikisha wanawakata baadhi ya watu wasio waaminifu wanaoiba miundombinu ya barabara.

“Naomba tushirikiane kuwafichua na kuwakamata watu wanaoiba miundombinu ya barabara,na tukiwakamata tuwafikishe katika vyombo vya sheria”,aliongeza Haule.

Aidha alitumia fursa hiyo kuwakumbusha akina mama kukaa mkao wa kiume wanapopanda pikipiki ama baiskeli badala ya kukaa upande upande ili kupunguza ajali za barabarani.

Naye Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Shinyanga,Anthony Masanzu alisema katika wiki hiyo ya nenda kwa usalama,wamefanikiwa kutoa elimu ya usalama barabarani kwa waendesha bodaboda 184.

Alisema mbali na kutoa elimu kwa waendesha bodaboda na wananchi waliotembelea mabanda ya usalama barabarani pia walitembelea shule mbalimbali mjini Shinyanga ambazo zipo karibu na barabara.

“Tumetumia wiki hii kutoa elimu ya usalama barabarani kwa makundi mbalimbali ya watumiaji wa barabara ili kuhakikisha kuwa tunazuia ajali na kuokoa maisha yao”,aliongeza Masanzu.

ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule akizungumza wakati wa kufunga wiki ya nenda kwa usalama barabarani mkoa wa Shinyanga mwaka 2017-Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule akisisitiza watumiaji wa barabara kuzingatia sheria za usalama barabarani ili kuepuka ajali
Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Shinyanga,Anthony Masanzu akizungumza wakati wa kufunga wiki ya nenda kwa usalama barabarani mkoa wa Shinyanga
Mwenyekiti wa kamati ya usalama barabarani mkoa wa Shinyanga,Wilson Majiji akizungumza wakati wa kufunga wiki ya nenda kwa usalama barabarani mkoa wa Shinyanga
Kwaya ya AICT Kambarage ikitoa burudani ya wimbo unaohusu masuala ya usalama barabarani
Wanafunzi wa shule ya msingi Town wakiimba wimbo  unaohusu  usalama barabaraniBurudani ya ngoma ya kucheza na nyoka ikiendelea


Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule akitoa vyeti kwa mmoja wa waendesha bodaboda (kati ya 184) waliopata mafunzo/elimu ya usalama barabarani wakati wa maadhimisho ya wiki ya nenda kwa usalama barabarani mkoa wa Shinyanga mwaka 2017.

Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527