TANZANIA KUNA MAPUNGUFU MAKUBWA KATIKA UTUNZAJI WA KUMBUKUMBU ZA WANAWAKE WALIOCHANGIA MAENDELEO YA TAIFA



Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP Mtandao,Vicensia Shule akizungumza na waandishi wa habari leo katika ukumbi wa TGNP Mtandao jijini Dar es salaam.
*****
Imebainika kuwa kuna mapungufu makubwa nchini katika utunzaji wa kumbukumbu hasa za wanawake wanaochangia maendeleo ya taifa licha ya kwamba wanawake wanachangia maendeleo bega kwa bega na wanaume. 

Akizungumza leo Septemba 8,2017 na waandishi wa habari wakati wa kuhitimisha tamasha la 14 la Jinsia mwaka 2017 lililoanza Septemba 5,2017, Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP Mtandao,Vicensia Shule alisema kumbukumbu za wanawake waliochangia maendeleo ya taifa hazijaandikwa. 

Alisema katika tamasha hilo lililokutanisha wadau zaidi ya 1500,wamekubaliana kuendelea kuimarisha mikakati ya kuweka kumbukumbu za wanawake waliotoa michango katika maendeleo katika nyanja mbalimbali. 

Shule alieleza kuwa mbali na kutunza taarifa hizo za kumbukumbu,pia watazisambaza kwa ajili ya watu kujifunza na kuwaenzi wanawake hao pamoja na kutoa mafunzo ya kimwongozo katika kuchukua na kuhifadhi kumbukumbu za wanawake kwa asasi za kiraia,vijana na wadau wengine. 

Hata hivyo alieleza kuwa kufuatia utafiti mdogo uliofanywa na TGNP Mtandao,walibaini kuwepo kwa wanawake waliochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya taifa na kupitia tamasha hilo TGNP iliwapatia wanawake hao tuzo ya kutambua michango yao. 

Shule aliongeza kuwa tuzo hizo ni sehemu ya mipango endelevu ya kurithisha ujuzi na maarifa kwa vizazi vipya pamoja na kujifunza kwa wanawake na wanaume waliobobea katika Nyanja maalum. 

Wanawake hao walikabidhiwa tuzo hizo na Makamu wa rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan wakati wa uzinduzi wa tamasha la Jinsia, Septemba 5,2017. 

Aliwataja wanawake waliopewa tuzo kuwa ni Mheshimwa Samia Suluhu,Getrude Mongella,Spika mstaafu wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Anne Makinda,Profesa Daktari Esther Mwaikambo,Anna Abdallah na Esther Bulaya. 

Wengine ni wanachama wa TGNP Mtandao waliotoa mchango mkubwa katika kujenga Tapo la Ukombozi wa wanawake kimapinduzi akiwemo Profesa Marjorie Mbilinyi,Asseny Muro,Mary Rusimbi,Demere Kitunga,Subira Kibiga,Aggripina Mosha na Zippora Shekilango. 

Na Kadama Malunde- Malunde1 blog
Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP Mtandao,Vicensia Shule(katikati)akizungumza na waandishi wa habari leo katika ukumbi wa TGNP Mtandao jijini Dar es salaam.Kushoto kwake ni Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP Mtandao,Lilian Liundi,kulia ni Mwenyekiti wa vituo vya taarifa na maarifa na mkurugenzi wa WAJIKI,Janeth Mawinza,wengine ni baadhi ya wadau wa masuala ya jinsia.

Waandishi wa habari wakimsikiliza Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP Mtandao,Vicensia Shule

Waandishi wa habari wakiwa ukumbini

Washiriki wa tamasha la jinsia mwaka 2017 wakicheza leo Septemba 8,2017 katika viwanja vya TGNP Mabibo jijini Dar es salaam
Washiriki wakicheza
Burudani inaendelea.
Picha zote na Kadama Malunde -Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post