Huduma Ya Treni Ya Abiria Kutoka Dar Kwenda Bara Kuanza Tena Jumapili Mei Mosi, 2016

Treni ya kwanza ya abiria ya Deluxe kutoka Dar es Salaam kwenda bara itaondoka saa 2 asubuhi siku Jumapili Mei Mosi, 2016 kuelekea Kigoma.


Kuanza kwa safari hiyo kunatokana na kutengemaa kwa eneo korofi baina ya stesheni za Kilosa mkoani Morogoro na Gulwe mkoani Dodoma.

Kwa mujibu wa taarifa ya Wakuu wa Idara za uendeshaji wa kampuni ya Reli Tanzania (TRL) iliyotolewa Aprili 26, 2016 baada ya ukaguzi wa kina wa eneo la Gulwe, imesema sasa eneo hilo linapitika na kwamba tuta limeiamarika na kuwezesha treni zote za abiria na mizigo kupita kwa usalama kabisa.


Mara ya mwisho huduma za treni za abiria ya kawaida zilihamishiwa Dodoma mnamo Aprili 07, 2016.


Ratiba za safari treni ya kawaida kutoka Dar es salaam kuelekea Mwanza na Kigoma ni kila siku ya Jumanne na Ijumaa saa 11 jioni ambayo imepangwa kuanza Jumanne Mei 3, 2016.Wakati treni ya Deluxe inaondoka Dar es salaam kila Jumapili saa 2.00 asubuhi.


Na kutoka Mwanza na Kigoma treni ya kawaida inatoka huko kila siku ya Alhamisi na Jumapili saa 11.00 jioni kwa Kigoma na saa 12 jioni kwa Mwanza. Treni ya DELUXE nayo inatoka Kigoma au Mwanza kila siku ya Jumanne saa 2.00 asubuhi.


Wasafiri wote wanaombwa kufanya mipango ya safari (booking) katika stesheni zetu husika na sio vinginevyo.


Aidha taarifa za uhakika kuhusiana na taratibu za safari zetu za treni za abiria na mizigo zinapatikana katika vituo vyetu vyote vya TRL.


Uongozi wa kampuni ya TRL unawaomba radhi wateja wake na wananchi kwa ujumla kwa usumbufu wowote uliojitokeza katika kipindi chote hicho ambacho huduma zetu zilipokuwa zinaanzia na kuishia Dodoma badala ya Dar es salaam kama ilivyo kawaida.


Aidha Kampuni inashukuru jitihada za Serikali pamoja na taasisi zake kadhaa kufanikisha kurejesha hali ya miundombinu ya reli katika hali yake ya kawaida.


Imetolewa na Afisi ya Uhusiano:
Kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TRL
Ndugu Masanja Kungu Kadogosa
Aprili 28, 2016
DAR ES SALAAM

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527