Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

BUNGE LAPITISHA BAJETI YA WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI


Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepitisha bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa mwaka wa fedha 2026/2027 baada ya kujadili na kuidhinisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo.

Awali, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mahmoud Thabit Kombo, aliliomba Bunge kupitisha jumla ya shilingi 359,326,404,000 ili kutekeleza majukumu ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Waziri Kombo alieleza kuwa kati ya fedha hizo, shilingi 312,961,378,000 zitatumika kwa Matumizi ya Kawaida, wakati shilingi 46,365,026,000 zimetengwa kwa ajili ya Bajeti ya Maendeleo.

Baada ya mjadala wa wabunge, Bunge limepitisha rasmi makadirio hayo ya bajeti kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Akiwasilisha bajeti ya Wizara hiyo Waziri Kombo alilieleza Bunge kuwa Tanzania imeendelea kudumisha misingi ya uhusiano na ushirikiano wa kimataifa, kama ilivyowekwa na waasisi wa Taifa na kuainishwa katika Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001, Toleo la 2024.

Alitaja Misingi hiyo kuwa ni Kulinda Mamlaka kamili ya nchi, mipaka kamili na uhuru wa kisiasa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Kulinda uhuru, haki za binadamu, usawa na demokrasia; Kukuza ujirani mwema; Kukuza Umoja wa Afrika; Kuongeza ushirikiano wa kiuchumi na washirika wa maendeleo; Kuwezesha utekelezaji wa sera ya kutofungamana na upande wowote na Ushirikiano wa nchi zinazoendelea; Kuunga Mkono Umoja wa Mataifa katika kuimarisha maendeleo ya kiuchumi, amani na usalama; na Kulinda maadili, mila, desturi na utamaduni wa watu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Misingi hii imechangia kudumisha heshima na taswira njema ya Taifa letu kupitia ushirikiano wa uwili, kikanda na kimataifa,” alisisitiza Balozi Kombo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com