Waganga wa tiba asili na tiba mbadala wanatarajia kukutana na Mkemia Mkuu wa Serikali ili kupatiwa elimu thabiti itakayowawezesha kuendelea kutoa huduma sahihi kwa jamii.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Chama cha Waganga wa Tiba Asili na Tiba Mbadala nchini (TAMESOT), Bw. Lukas Joseph Mlipu, alipokuwa katika Kata ya Butengorumasa mkoani Geita akiwahamasisha waganga kuhusu umuhimu wa kushiriki mafunzo yatakayotolewa na Mkemia Mkuu wa Serikali.
Amesema mafunzo hayo yanayowalenga waganga wote yana umuhimu mkubwa kutokana na changamoto mbalimbali zinazoikabili taaluma ya tiba asili. Ameeleza kuwa juhudi za serikali, ikiwemo utoaji wa elimu kwa wataalamu hao, zitasaidia kuboresha huduma za tiba asili na kuhakikisha zinaendeshwa kwa kuzingatia viwango vya kitaalamu.
Aidha, Bw. Mlipu amefafanua kuwa Mkemia Mkuu wa Serikali atatoa mafunzo hayo tarehe 23 Machi, 2026, mkoani Geita. Hivyo, ametoa wito kwa waganga wote kuhakikisha hawakosi fursa hiyo muhimu kwa mustakabali wa taaluma yao.



Social Plugin