Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

TBS YAPONGEZWA KWA KUSAIDIA WAJASIRIAMALI KUPATA ALAMA YA UBORA

Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro Dkt.Mussa Ali Mussa Akizungumza na baadhi ya wafanyakazi wa shirika la viwango Tanzania (TBS)katika vibanda vya nanenane Morogoro 

Na Mwandishi wetu Malunde 1 Blog-Morogoro 

Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Mussa Ali Mussa, amelipongeza Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kwa juhudi zake katika kuwahudumia wananchi, hususani wajasiriamali na wazalishaji wadogo, kwa kuwawezesha kupata alama ya ubora bila gharama yoyote.

Akizungumza katika Maonesho ya Nane nane yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Dkt. Mussa amesema huduma zinazotolewa na TBS ni muhimu kwa maendeleo ya taifa kwa kuwa zinahakikisha bidhaa zinazozalishwa ndani na nje ya nchi zinakidhi viwango vya ubora vinavyokubalika kitaifa na kimataifa.

“Kupitia TBS, bidhaa zetu zinaendelea kupata ushindani katika masoko ya kikanda na kimataifa. 

Hili ni jambo muhimu kwa uchumi wetu na kwa maendeleo ya wajasiriamali wetu,” amesema Dkt. Mussa.

Aidha, amelitaka shirika hilo kuendelea kushirikiana kwa karibu na wadau wa sekta ya kilimo na viwanda katika kutoa elimu kwa wakulima na wazalishaji ili waweze kuongeza thamani ya bidhaa zao kwa kuzingatia viwango vya ubora.

Kwa upande wake, Afisa Udhibiti Ubora Mwandamizi wa TBS Kanda ya Mashariki, Sileja Lushibika, amesema shirika linaendelea kupanua huduma zake kwa kuhakikisha linawafikia wadau kupitia ukaguzi wa bidhaa viwandani na sokoni, utoaji wa mafunzo, pamoja na elimu kupitia vyombo mbalimbali vya habari.Lushibika amesema TBS inawasaidia wajasiriamali kupata alama ya ubora bila malipo kwa kipindi cha miaka mitatu, ambapo wanapaswa kuwasilisha barua ya utambulisho kutoka Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO).

 “Tunatumia Maonesho haya kama jukwaa muhimu la kutoa elimu kwa umma kuhusu uzalishaji wa bidhaa bora, kuonyesha teknolojia mpya, na kubadilishana uzoefu na wadau mbalimbali wa sekta ya viwanda na biashara,” ameongeza Lushibika.

TBS ni miongoni mwa taasisi za Serikali zinazoshiriki Maonesho ya Nane nane mwaka huu, yakihusisha wakulima, wazalishaji na taasisi mbalimbali za maendeleo kutoka mikoa yote ya Kanda ya Mashariki.




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com