MWANDISHI WA HABARI TANGA TV, DEREVA MAMLAKA YA MAJI TANGA WAFARIKI KWA AJALI KWENYE MSAFARA




Na Hamida Kamchalla, TANGA.


WATU wawili wamefariki dunia na wengine wawili wamejeruhiwa vibaya leo mkoani Tanga baada ya gari waliyokuwa wakisafiria kwenye msafara wa Naibu Waziri Mkuu Dkt. Dotto Biteko alipokuwa kwenye ziara ya kikazi katika Mkoa huo.


Ajali hiyo ilitokea majira ya saa 3 asubuhi katika kijiji cha Mamboleo, Wilaya ya Muheza wakati msafara huo ukitokea jijini Tanga kuelekea wilayani Korogwe kukagua mradi wa kufua umeme katika mji wa Hale.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga ACP Almachius Mchunguzi amethibitisha ajali hiyo na kuwataja marehemu kuwa ni Ally Hassan, Mwandishi wa habari wa TV ya halmashauri ya jiji la Tanga na Saidi Alawi, dereva wa Mamlaka ya Maji Tanga (TANGA Uwasa).


Aidha amewataja majeruhi kuwa ni Frank Godfrey, mwandishi wa habari wa AYO TV pamoja na Mhandisi wa Maji wa TANGA Uwasa, Salum Ng'umbi ambao wako katika hospitali ya Rufani ha Bombo mkoani humo.


"Gari hiyo ilikuwa kwenye msafara wa Naibu Waziri Mkuu, ni mali ya idara ya maji mkoani Tanga, aina ya Toyota Hilix, DFPA - 9631, ambapo gari iliacha njia na kupinduka, majeruho wako hospitali ya Bombo wanaendelea kupatiwa matibabu.


Naye Mganga Mfawidhi wa hospitali ya Bombo, Dkt. Frank Shega amekiri kupokea wahanga hao majira ya nne kasoro ambapo watatu walikuwa katika hali mbaya na mmoja alikuwa tayari ameshaaga dunia.


"Nimepokea majeruhi watatu na mwengine alikuwa ameshafariki, wakati wanapatiwa matibabu mmoja nae akafariki, lakini hali za majeruhi ni mbaya ambapo mmoja amesafirishwa kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili na mwengine alikimbizwa chumba cha upasuaji,


"Huyu aliyepelekwa Muhimbili ni mhandisi wa maji TANGA Uwasa, amepata tatizo la mifupa na mwengine mwandishi wa habari baada ya vipimo imeonesha damu imemwagikia ndani, Madaktari wanaendelea kupigania maisha yake" amesema Dkt. Shega.


INNALILLAH WAINNA ILAYHI RRAJIUN. / BWANA AMETOA NA BWANA AMETWAA, JINA LAKE LIHIMODIWE...AMIN.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post