EWURA YAVIPIGA PINI VITUO VIWILI VYA MAFUTA NCHINI



MENEJA Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) Bw. Titus Kaguo,akisitiza jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) leo Septemba 30,2023 jini Dodoma wakati akitoa taarifa kuhusu kuvifungia vituo viwili vya mafuta nchini kwa kosa la kuhodhi mafuta.


Na.Alex Sonna-DODOMA

MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imevifungia vituo vingine viwili vya mafuta kwa kosa la kuhodhi mafuta, kati ya mwezi Julai na Agosti 2023, Vituo hivyo ni Rashal Petroleum Ltd-Mlimba, Mkoa wa Morogoro na Kimashuku Investment Co. Ltd-Babati, Mkoa wa Manyara.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Septemba 30,2023 jijini Dodoma Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka EWURA Bw. Titus Kaguo,amesema kuwa hatua zilichukuliwa kwa vituo vyote vilivyobainika kuficha mafuta na kusababisha uhaba wa bidhaa hiyo nchini.
Bw,Kaguo amesema kuwa kuanzia mwezi Julia mwaka huu kumekuwepo na matukio kwa baadhi ya maeneo ya pembezoni mwa nchi kukosa mafuta hasa kipindi bei zinapoelekea kubadilishwa na kusababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi na madhara ya kiuchumi.


"Kama tulivyoeleza katika mkutano na waandishi wa habari tarehe 18 mwezi huu kule Dar es Saalam EWURA iliendelea na uchunguzi wa vituo vingine ikiwemo kupata fursa ya kuwasilisha utetezi wao ndani ya siku 21"amesema Bw,Kaguo

Amesema kuwa baada ya kupitia utetezi wao katika kikao cha Septemba 2023 Bodi ya wakurugenzi wa EWURA ilijiridhisha pasipo shaka kuwa vituo viwili vilitenda kosa la kuhodhi mafuta kati ya mwezi Julai na Agosti 2023.

"Hivyo kuamua vifungiwe kwa kipindi cha miezi sita vituo hivyo ni Rashal Petroleum Ltd-Mlimba mkoani Morogoro na Kimashuku Investment Co. Ltd-Babati mkoa wa Manyara"amesema Bw,Kaguo

Hata hivyo amesema EWURA inawakumbusha wafanyabishara wote wa mafuta nchini kuhakikisha wanaendesha biashara zao kwa mujibu wa sheria,kanuni na miongozo inayosimamia biashara hiyo.

"EWURA inatoa onyo kwa OMCs na wamiliki wa vituo vya mafuta kuwa serikali inafuatilia suala hili kwa karibu kupitia vyombo vyake mbalimbali na kuwa ikidhibitika uvunjaji wa sheria na kanuni umetendeka hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao ikiwemo kuwafutia leseni zao za biashara"amesisitiza
MENEJA Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) Bw. Titus Kaguo,akizungumza na waandishi wa habari leo Septemba 30,2023 jini Dodoma kuhusu kuvifungia vituo viwili vya mafuta nchini kwa kosa la kuhodhi mafuta.

MENEJA Mawasiliano na Uhusiano wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) Bw. Titus Kaguo,akisitiza jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) leo Septemba 30,2023 jini Dodoma wakati akitoa taarifa kuhusu kuvifungia vituo viwili vya mafuta nchini kwa kosa la kuhodhi mafuta.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post