MBUNGE BYABATO ATOA MSAADA WA MAJIKO YA GESI KWA MAMA LISHE, TV KWA WAFANYABIASHARA SOKO KUU BUKOBA


Na Mariam Kagenda - Bukoba

Katika jitihada za kuhakikisha anarudisha shukrani kwa wananchi waliomchagua mbunge wa Jimbo la Bukoba mjini ambaye pia ni Naibu Waziri wa Nishati Wakili Stephen Byabato ametoa msaada wa Television 6 kwa wafanyabiashara wa soko kuu la Bukoba na majiko 28 ya gesi kwa mama lishe.


Mhe. Byabato amekabidhi Television pamoja na majiko ya gesi Agosti 11, 2023 na kuwasha Television hizo jambo ambalo litawasaidia wafanyabiashara wa soko hilo kutopitwa na habari za matukio mbalimbali yanayoendelea ndani na nje ya nchi.


Akizungumza na wafanyabiashara hao amesema kuwa amenunua Television hizo ikiwa ni shukrani zake kwa wafanyabiashara wa soko kuu na kuhakikisha hawapitwi na taarifa ya habari, mpira na hotuba za viongozi wa Kitaifa akiwemo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na matukio mengine yanayoendelea ndani na nje ya nchi.


Ameongeza kuwa Television hizo wanaweza kuzitumia kuangalia vipindi vya bunge pamoja na vipindi mbalimbali cha kuelimisha jamii juu ya maswala ya afya,elimu na kilimo.


Tukio hilo limehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Chama Cha Mapinduzi na serikali akiwemo mstahiki Meya na madiwani .


Kwa upande wao wafanyabiashara wa soko kuu wamemshukuru Mhe. Mbunge Stephen Byabato kwa kuona umuhimu wa kupeleka Television katika soko hilo na kuomba afikishe salamu zao za shukrani na pongezi kwa Rais Samia Suluhu Hassan.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post