TBS YAHIMIZA WANANCHI KUTUMIA CHAKULA SALAMA KULINDA AFYA ZAO

Kaimu Meneja Kitengo cha Tathmini ya Viatarishi vya chakula TBS, Dkt.Ashura Kilewela akizungumza na waandishi wa habari leo Mei 25,2023 kwenye ofisi za TBS Jijini Dar es Salaam

*****************

KATIKA kuelekea kwenye Maadhimisho ya Siku ya Chakula Salama, TBS inawakumbusha wananchi kutumia chakula salama hasa katika uzingatiaji kwenye uandaaji kwa kutumia malighafi safi pamoja na utunzaji wa chakula.

Maadhimisho hayo hufanyika kila ifikapo tarehe 7 Juni kila mwaka ambapo kauli mbiu ya mwaka huu ni 'Viwango vya Chakula Huokoa Maisha'.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Mei 25,2023 Jijini Dar es Salaam, Kaimu Meneja Kitengo cha Tathmini ya Viatarishi vya chakula TBS, Dkt.Ashura Kilewela amesema viwango vya uhakika huokoa maisha na ni muhimu katika maisha yetu ya kila siku hivyo basi tuhakikishe tunatumia chakula salama kulinda afya zetu.

"Uandaaji wa chakula salama ni jukumu letu sote, kwahiyo ili tuwe na chakula salama kila mmoja anatakiwa kutumia kiwango vile inavyotakiwa ". Amesema

Amesema maadhimisho ya mwaka huu TBS inategemea kuwashirikisha wananchi na wadau mbalimbali katika kusheherekea maadhimisho hayo lengo kubwa ni kutoa elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa matumizi ya chakula salama.

"Lengo la maadhimisho haya ni kuinua uelewa wa jamii juu ya chakula salama kwasababu ukila chakula salama utakuwa na afya bora na utaweza kufanya majukumu yako ya kila siku". Amesema Dkt.Kilewela.

Hata hivyo amesema kuwa wanapoelimisha jamii wanasaidia kuepukana na madhara yanayopatikana na ulaji wa chakula kisicho salama.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments