NAIBU WAZIRI ASISITIZA KAMPUNI ZA MADINI KUTOA FURSA ZA AJIRA, ZABUNI KWA WATANZANIA

Mfanyakazi wa Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML), Omary Faustine Matulanya akitoa maelezo kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Patrobas Katambi (kushoto) kuhusu matairi yanayotumika kwenye mitambo ya ubebaji  mawe na mchanga wa dhahabu kutoka ndani ya migodi. Katambi alitembelea banda la kampuni hiyo kwenye maoneosho ya afya na usalama mahali pa kazi yaliyofanyika kwenye viwanja vya Tumbaku mkoani Morogoro kuanzia tarehe 26 hadi 30 Aprili mwaka huu.
Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Prof. Joyce Ndalichako akisalimiana na baadhi ya wafanyakazi wa kampuni ya GGML alipotembelea banda la kampuni hiyo kwenye maonesho ya afya na usalama mahali pa kazi yaliyofikia tamati tarehe 30 Aprili 2023.
Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Prof. Joyce Ndalichako akisalimiana na baadhi ya wafanyakazi wa kampuni ya GGML alipotembelea banda la kampuni hiyo kwenye maonesho ya afya na usalama mahali pa kazi yaliyofikia tamati tarehe 30 Aprili 2023.
Baadhi ya wafanyakazi wa Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) wakiwa kwenye picha ya pamoja na Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Prof. Joyce Ndalichako ambaye juzi Jumapili alitembelea banda la kampuni hiyo katika maonesho ya wiki ya afya na usalama mahali pa kazi na kufanyika kwenye viwanja vya Tumbaku mjini Morogoro. Katika maonesho hayo GGML imeibuka mshindi wa jumla kama muoneshaji bora na kampuni bora yenye ubunifu wa vifaa vya kisasa vinavyozingatia afya na usalama mahali pa kazi.



NA MWANDISHI WETU, MOROGORO

NAIBU Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na watu wenye Ulemavu, Patrobas Katambi ameipongeza Kampuni ya Geita Gold Mining Limited (GGML) kwa kutoa fursa za ajira kwa Watanzania zaidi ya asilimia 90 ndani ya mgodi huo pamoja na kuwapatia wazawa fursa za kutoa huduma za kuuza bidhaa za ndani kwenye kampuni hiyo.



Pia ameipongeza kampuni hiyo kwa kuibuka mshindi wa ubunifu na banda bora kwenye maonesho ya afya na usalama mahali pa kazi yaliyofanyika katika viwanja vya Tumbaku mkoani Morogoro kuanzia tarehe 26 hadi 30 Aprili mwaka huu.

Katambi alitoa pongezi hizo mwishoni mwa wiki alipotembelea banda la kampuni hiyo katika maonesho hayo yaliyoratibiwa na Wakala wa Afya na Usalama mahali pa kazi (OSHA).


“Niwapongeze hasa kwa kupunguza ulemavu kazini, magonjwa yanayotokana na kazi lakini pia kuhakikisha kwamba mazingira yote ya kufanyia kazi yanakuwa salama.


“Nafurahi kuona kwamba banda zima na hata ndani ya kampuni asilimia kubwa ya wafanyakazi ni watanzania wenzetu kwa maana hiyo tunazidi kusisitiza kwamba kwenye maeneo yote ya kazi watanzania ni kipaumbele,” alisema.


Alisema mgeni anaposhika nafasi ya ajira ina maana kwamba ujuzi huo ni adimu, mtanzania hana sifa wala vigezo lakini pamoja na hilo Rais Samia Suluhu Hassan ameelekeza watanzania wajengewe uwezo kushika nafasi hizo.

“Ameelekeza kuhakikisha wakati wote kwamba wakiwepo wageni wenye ujuzi nyuma yake awepo mtanzania anayejifunza hizo kazi na baada ya muda, utaalamu tubaki nao wenyewe,” alisema.


Alisema GGML imekuwa mfano wa kuigwa katika manunuzi yanayofanyika kwenye migodi yake kwa sababu Serikali kupitia mpango wa kuwezesha wazawa kutoa huduma na kuuza bidhaa ndani ya mgodi (local content) inasisitiza kwamba vitu kama vipo hapa nchini vinunuliwe hapa hapa ili kiuongeza ukwasi ndani ya nchi ili fedha nyingi isitoke nje.

“Lakini pia mmezingatia usalama wa mazingira kwa ujumla ili tusipate watu wenye ulemavu unaotokana na migodi hata pia mazingira na ardhi yetu inabaki kuwa salama kwa hiyo nyinyi watanzania mliopo huko ni wawakilishi wa kuhakikisha usalama unakuwepo...wa kwetu sisi, viumbe hai,” alisema.

Aidha, akimkaribisha katika banda hilo, Meneja anayehusika na usalama kazini kutoka GGML, Isack Senya alisema zaidi ya wananchi 3000 wametembelea banda hilo na kujifunza mambo mbalimbali kuhusu teknolojia zinazotumika kufanya kazi katika mazingira yenye afya na usalama.


Alisema mwaka huu GGML ilileta vifaa vya kiteknolojia na kisasa kiasi cha kuiwezesha kampuni hiyo kuibuka kampuni bora yenye ubunifu kwenye vifaa hivyo.

Pia alimuahidi Naibu Waziri kuendelea kutekeleza miradi mbalimbali inayosaidia jamii kuondokana na umaskini pamoja na kupata huduma bora kwa kushirikiana na serikali.

Pamoja na mambo mengine, Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na watu wenye Ulemavu, Prof. Joyce Ndalichako naye alipita katika banda hilo na kuipongeza kampuni hiyo kwa kuwa mdau muhimu katika kuzingatia matakwa ya sheria yanayosisitiza afya na usalama mahali pa kazi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments