TANROADS KUPITIA WAKANDARASI WAZAWA, YAKAMILISHA UJENZI WA BARABARA KWA KIWANGO CHA LAMI RUDEWA-KILOSA (KM 24)


Na Mwandishi Wetu, Morogoro 

Mradi wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami Dumila-Kilosa-Mikumi sehemu ya LUDEWA-KILOSA yenye urefu wa kilometa 24 umefikia asilimia 90 ambapo mradi huo unatarajiwa kukamilika Julai, mwaka huu.

Kazi iliyobakia ni ujenzi wa madaraja matatu huku ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami ikiwa imekamilika na kuendelea kutumika.

Hayo yamesemwa Aprili 16, 2023 na Kaimu Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Morogoro Mhandisi Mussa Kaswahili akitembelea miradi ya Ludewa-Kilosa na daraja la Kiyegeya lililopo wilayani Gairo ambapo amesema barabara hiyo ni sehemu ya barabara ya mkoa huo ambayo inaanzia Dumila hadi Mikumi.

Mhandisi Kaswahili ameongeza kuwa, hapo awali watumiaji wa barabara hiyo walikuwa wanatumia muda mrefu barabarani hadi kufika wakitokea Dumila kwenda Rudewa au Kilosa kutokana na ubovu wa barabara iliyokuwepo.

"Hapo awali kabla ya ujenzi wa barabara ya Dumila hadi Kilosa, ilikuwa kutoka Dumila hadi Ludewa ilikuwa ni masaa matatu lakini kwa sasa ni takribani dakika 40 tu unakuwa umefika" alisema Mhandisi Kaswahili.

Mhandisi Kaswahili ameendelea kwa kusema kuwa, mradi wa Ludewa-Kilosa ulibuniwa ili kuwajengea uwezo wakandarasi wazawa katika kuongeza ushiriki wako kwenye miradi ya ujenzi wa miundombinu.


"Mradi wa Ludewa-Kilosa ulibuniwa ili kuwajengea uwezo wakandarasi wazawa, katika mradi kuna wakandarasi 7 walioungana na kuunda Umoja Kilosa JV lengo ni kutumia wakandarasi wazawa badala ya kutumia wakandarasi wa kigeni hapo baadaye" alisisitiza Mhandisi Kaswahili

Wakiongea kwa nyakati tofauti, Meneja wa mradi LUDEWA-KILOSA kutoka kampuni ya ushauri ya Pidael JV Consulting Engineers Mhandisi Protas Mwasyoke na msimamizi wa mradi upande mkandarasi, Mhandisi Leons Msoka wamesema kwa mwenendo wa kazi za ujenzi zinavyoendelea na kwa kazi ikiyobakia ya ujenzi wa madaraja matatu, kazi hiyo itakamilika kwa wakati mwezi Julai, mwaka huu.

Akiwa katika daraja jipya la Kiyegeya wilayani Gairo, Mhandisi Kaswahili emeeleza kuwa, daraja hilo limejengwa kwa viwango na teknolojka ya kisasa na kumaliza kabisa changamoto iliyokuwa ikitokea hapo zamani hususan nyakati za mvua na hata kupelekaa daraja la zamani kubomoka na kuathiri shughuli za usafiri na usafirishaji.

Kufuatia hatua hiyo, serikali iliiingia katika mpango wa dharura na kutenga fedha haraka kwa ajili ili kujenga daraja jipya la Kiyegeya chini ya usimamizi wa Kitengo cha wahandisi washauri wa TANROADS Mkoa wa kwa kushirikiana na TANROADS makao makuu.

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa daraja la kisasa la Kiyegeya Mhandisi Kaswahili amesema,

"Ujenzi wa daraja la Kiyegeya limegharimu kiasi cha shilingi bilioni 6.9 ambao mradi wa ujenzi wa daraja hilo ulikamilika Februari 28, 22022 na linatumika kwa asilimia 100 na kuongeza kuwa

"Nipende kuishukuru serikali ya awamu sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutenga na kuleta fedha ili miradi ya kimkakati ikiwemo mradi huu (ujenzi wa daraja la Kiyegea) iweze kutekelezwa na kufungua shughuli za uchumi za nchi na kwa mwananchi mmoja mmoja"

Mkoa wa Morogoro una madaraja takriban 2,029 huku mtandao wa barabara ukiwa takriban kilometa 2070. Serikali inaendelea kutenga fedha ili kuhakikisha barabara hizo zinahudumiwa ili kuweza kuhakikisha kwamba zinapitika muda wote na majira yote ya mwaka.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments