TBS YAADHIMISHA SIKU YA VIWANGO BARANI AFRIKA



WAFANYABIASHARA wadogo na wa kati wanakabiliwa na changamoto kadhaa,zikiwemo mitaji midogo, teknolojia duni, elimu ndogo ya masuala ya ujasiriamali, elimu ndogo kuhusiana masuala ya ubora na usalama na pia kukosekana kwa masoko ya uhakika ambapo kwa kiasi kikubwa huwadumaza. 

Ameyasema hayo jana Machi 28,2023 Mkuu wa Wilaya ya Mbeya Mhe.Beno Malisa kwa niaba ya mkuu wa Mkoa wa Mbeya katika Maadhimisho ya Siku ya Viwango Afrika, yaliyofanyika katika ukumbi wa Beaco, Jijini Mbeya. 

Amesema kuwa ni ukweli usiopingika kwamba wajasiriamali wadogo na wa kati wanapokuwa katika mazingira ya changamoto mbalimbali hawawezi kuchangia ipasavyo katika maendeleo, kutokomeza umaskini na kukuza viwanda na uchumi wa Taifa kwa ujumla. 

"Ni wazi kuwa wakiendelezwa na kuondolewa changamoto zinazowakabili watachangia kwa kiasi kikubwa katika mipango ya Taifa ya kuondoa umaskini, kujenga ustawi wa jamii na kukuza uchumi". Amesema 

Pamoja na hayo amesema wajasiriamali wadogo na wa kati hawawezi kufikia malengo yao iwapo watapuuza masuala ya ubora na usalama katika uzalishaji wao. 

Amesema kwa mujibu wa takwimu za Chama cha Wafanyabiashara, Wenye Viwanda na Wakulima Tanzania (TCCIA), asilimia 95 ya biashara zinazofanyika nchini ni biashara za wajasiriamali wadogo na wa kati, ambazo huchangia takriban asilimia 35 ya Pato la Taifa (GDP) na kuzalisha hadi asilimia 40 ya ajira. 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Uandaaji Viwango (TBS), Bw.David Ndibalema amesema mbali na mafunzo na elimu ambayo hutolewa mara kwa mara kwa wajasiriamali wadogo, wa kati na umma kwa ujumla, Serikali hutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya kuhudumia wajasiriamali wadogo na wa kati pale wanapoomba kuthibitisha ubora wa bidhaa zao. 

"Anachotakiwa kuwa nacho mjasiriamali huyu mdogo ni leseni ya biashara na barua ya utambulisho kutoka Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) ambapo TBS hupokea barua hiyo na kuendelea na taratibu zingine za uthibitishaji ubora". Amesema 

Amesema tangu kuanza kwa utaratibu huo, tumefanikiwa kuthibitisha ubora wa bidhaa za wajasiriamali 1,515 nchini kote na wengine wengi wako katika hatua mbalimbali za michakato ya kupata leseni ya kutumia alama ya ubora.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments