SHINDANISHENI TAFITI ZENU ILI ZIWEZE KUPATA SOKO EAC-PROF.MSHANDETE


Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Elimu, Utafiti na Ubunifu kutoka Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Profesa Anthony Mshandete akisisitiza jambo wakati wa ufunguzi wa Shindano la Wazo la Kibiashara lililoandaliwa na Ndaki ya Biashara na Sayansi ya Jamii (BuSH) kwa udhamini wa Taasisi hiyo na Chuo cha Washington State cha nchini Marekani Machi 3,2023.


Washiriki wa Shindano la wazo la Kibiashara lililoandaliwa na Ndaki ya Biashara na Sayansi ya Jamii (BuSH) kwa udhamini wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela na Chuo cha Washington State cha nchini Marekani wakifuatilia matukio katika shindano hilo lilifanyika Machi 3,2023.


Washindi wa kwanza katika Shindano la wazo la biashara la Kifaa Kinachotumia nishati ya mwanga wa jua kutambua uwepo wa vimelea vya TB kwenye mazingira hatarishi ambao ni Clarence Rubaka, Happiness Mkumbo, Angela Aluko na Kelvin Makuki wakiwa katika picha ya pamoja na waratibu wa shindalo hilo.


Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Elimu, Utafiti na Ubunifu kutoka Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Profesa Anthony Mshandete (Katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa wazo la Kibiashara.



Na.Mwandishi Wetu-ARUSHA

Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Elimu, Utafiti na Ubunifu kutoka Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Profesa Anthony Mshandete ametoa wito kwa watafiti na wanazuoni kushindanisha tafiti zao ili ziweze kuwa bidhaa na huduma zenye ushindani wa soko la nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

Profesa Mshandete ameyasema hayo Machi 3,2023 Jijini Arusha wakati akifungua shindano la Ubunifu wa Biashara liloshirikisha makundi manne ya watafiti wanafunzi kutoka taasisi hiyo chini ya uratibu wa Ndaki ya Biashara na Sayansi ya Jamii (BuSH) kwa udhamini wa Taasisi hiyo na Chuo cha Washington State cha nchini Marekani.

“Shindano hili ni muhimu katika kuwahamasisha watafiti walioko vyuoni na katika taasisi kutoa tafiti zenye kukidhi viwango, na kuzitoa katika maabara ziwe bidhaa zitakazoingia sokoni ili kuleta ajira kwa vijana na ushindani katika soko la Afrika Mashariki” amesema Profesa Mshandete.

Amesema kuwa washiriki hao wanatakiwa kutumia fursa hiyo, katika kutoa tafiti zenye kuleta matokeo chanya ili kupata suluhisho katika kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii.

Naye Mmoja wa Majaji katika shindano hilo Privanus Katinhila ameipongeza Taasisi ya Nelson Mandela, kwa kuratibu shindano hilo katika tasnia ya viwanda, biashara na uwekezaji na kutoa rai kwa wafanyabiashara wa jiji la Arusha, kuitumia Taasisi hiyo kujifunza fursa mbalimbali zinazopatikana ikiwemo tafiti na bunifu ili kuwezesha bidhaa zao kuwa na ubora zaidi.



Washindi wa kwanza katika Shindano hilo ni Clarence Rubaka, Happiness Mkumbo, Angela Aluko na Kelvin Makuki wenye wazo la kibiashara la Kifaa Kinachotumia nishati ya mwanga wa jua kutambua uwepo wa vimelea vya TB kwenye mazingira hatarishi ambapo wamejipatia zawadi ya shilingi milioni tatu pamoja na nafasi ya mafunzo ya wiki mbili katika Chuo cha Washington State nchini Marekani ili kuboresha zaidi wazo hilo la Kibishara huku washindi wa pili wakipata shilingi milioni mbili na washindi wa tatu shilingi milioni moja.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments