MCHENGERWA, DKT. ABBASI WATETA NA WADAU WA UWINDAJI NA TAWA


Na John Mapepele

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mohamed Mchengerwa leo amekutana na wataalam wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) na Chama cha Wawindaji Wenyeji na kufanya kikao cha kazi kilicholenga kuleta mapinduzi makubwa ya kiutendaji.

Kikao hicho cha kimkakati kilihudhuriwa pia na Katibu Mkuu, Dkt. Hassan Abbasi, ambapo pamoja na mambo mengine kimejadili namna bora kuboresha utendaji wa kazi, uhifadhi wa maeneo, uwindaji, utatuzi wa migogoro na mipaka na utalii.

Katika kikao hicho, Mhe. Waziri ameagiza maelekezo kadhaa kwa TAWa ambayo ametaka yafanyiwe kazi kwa haraka ili kuboresha uhifadhi kwa faida ya vizazi vya sasa na baadaye na kutangaza vivutio vya utalii.

Amewataka wataalam kufanya kazi kibiashara ili kuwavutia wawekezaji badala ya kufanya kazi kwa mazoea huku wakijiepusha na vitendo vya upendeleo, rushwa na dhuluma.

Aidha, amewataka kuwa wabunifu, kufanya kazi kwa weledi na kuwa wazalendo kwa nchi yao.

Mwenyekiti wa Umoja wa Wawindaji Wenyeji Japhari Mohamed amemshukuru Mhe. Waziri kwa kufungua milango kwa wadau mbalimbali kukutana na kujadiliana nao.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments