ASKARI POLISI AKUTWA AMEFARIKI KWENYE NYUMBA YA KULALA WAGENI ARUSHA NDUGU WAKIMUUA KIJANA ALIYETUKANA MAMA YAKE MZAZI

Na mwandishi wetu Jeshi la Polisi

Jesh la Polisi mkoa wa Arusha limesema kuwa tarehe 08 Januari mwaka huu Jeshi hilo lilipokea taarifa ya matukio ya watu wawili kufariki dunia katika maeneo tofauti tofauti katika Mkoa wa Arusha.


Akitoa taarifa hiyo  leo Januari 11 kamanda wa Palisi Mkoa wa Arusha kamishina Msadizi wa Polisi ACP JUSTINE MASEJO amesema kuwa Tarehe 08.01.2023 muda wa saa 08:30 usiku Jeshi la Polisi Mkoani hapa lilipokea taarifa ya uwepo wa mtu mmoja ambaye alifariki maeneo ya nyumba ya kulala wageni ijulikanayo kwa jina la Mrina Shine iliyopo kata ya Levolosi Jijijini Arusha.


Kamanda Masejo amebainisha kuwa mara baada ya kupokea taarifa hiyo, Polisi walifika eneo hilo na kuukuta mwili huo ambao waliutambua kuwa ni Mkaguzi wa Polisi Stewart Kaino (47) Askari Polisi wa wilaya ya Arumeru.


Aidha amesema kuwa jeshi hilo bado linaendelea na uchunguzi wa kina ili kubaini mazingira mazima ya kifo hicho.


Sambamba na hilo Kamanda Masejo ameelezea tukio jingine ambapo amesema  kuwa Tarehe 08.01.2023 huko katika Hospitali ya Rufaa ya Mount Meru Arusha mtu mmoja aitwaye Nelson Mollel (33) mfanyabiashara, mkazi wa kata ya Moivo, Wilaya ya Arumeru na Mkoa wa Arusha alifariki dunia wakati akiendelea kupatiwa matibabu baada ya kujeruhiwa kwa kupigwa.


ACP MASEJO amebainisha kuwa Uchunguzi wa awali wa Jeshi hilo umebaini kuwa mtu huyo alifariki dunia baada ya kujeruhiwa kwa kupigwa na watu wanaodaiwa kuwa ni ndugu zake tarehe 03.01.2023 wakimtuhumu kumtukana mama yake mzazi (jina limehifadhiwa) na kumuibia.



Kamanda Masejo aliendelea kufafanua kuwa baada ya kupigwa, ndugu hao waliendelea kukaa na majeruhi bila kumpeleka hospitali hadi ilipofika tarehe 08.01.2023 alifikishwa hospitali akiwa mahututi na kufariki dunia wakati akiendelea kupatiwa matibabu.


Amesema kuwa Jeshi hilo linaendelea na upelelezi ili kuwakamata watu wote waliohusika katika tukio hilo ambao walikimbia baada ya kuona hali ya marehemu kuwa mbaya.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments