LIKIZO KWA WATUMISHI WA UMMA NYAKATI ZA SIKUKUU ZISIWE KIKWAZO CHA KUWAHUDUMIA WANANCHI-Mhe. Ndejembi

Na. Veronica E. Mwafisi-Kinondoni

Tarehe 13 Disemba, 2022

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema likizo za mwaka kwa watumishi wa umma katika kipindi cha sikukuu zisiwe kikwazo cha kutoa huduma kwa wananchi.

Akizungumza na Watumishi wa Umma wa Manispaa ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam, Mhe. Ndejembi amesema, likizo ya mwaka ni haki ya mtumishi lakini inatakiwa kuchukuliwa kwa tahadhari hasa katika kipindi cha sikukuu ili isiathiri utoaji wa huduma kwa wananchi wanaofuata huduma katika taasisi za Serikali.

Mhe. Ndejembi amesema watumishi wanapochukua likizo kipindi cha sikukuu, ni vema baadhi wakabaki ofisini ili kuendelea kutoa huduma kama kawaida kwani wananchi wanahitaji huduma nyakati zote za sikukuu na za kawaida.

“Tuhakikishe huduma zinatolewa kama kawaida katika vituo vyetu vya kazi katika kipindi hiki cha Sikukuu kama zinavyotolewa katika siku za kawaida kwani serikali hailali, hufanya kazi wakati wote,” Mhe. Ndejembi amesisitiza.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka watumishi wa umma nchini kujitathmini kiutendaji kwa kujiwekea malengo kupitia watumishi binafsi, Idara na Taasisi kwa ujumla katika kutekeleza majukumu yao ya kuwahudumia wananchi ili kuunga mkono kwa vitendo Kaulimbiu ya Kazi Iendelee ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kinondoni, Bi. Stella Msofe amemshukuru Mhe. Ndejembi kwa kuhimiza uwajibikaji, kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali ya kiutumishi ikiwa ni pamoja na kutatua kero na changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiwakabili watumishi walio katika wilaya yake.

Bi. Msofe, ameahidi kusimamia utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Naibu Waziri aliyoyatoa kwa watumishi kwa kushirikiana na wasaidizi wake kuanzia ngazi ya Kata, Mtaa na Halmashauri kwa ujumla.

Naye, Mtumishi wa Manispaa ya Kinondoni, Bi. Happyfania Mabala amemshukuru Mhe. Ndejembi kwa kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali ya kiutumishi, ikiwa ni pamoja na kutatua kero na changamoto zilizokuwa zikiwakabili watumishi wa Halmashauri hiyo kwa muda mrefu.

Kadhalika, Bi. Mabala ameushukuru uongozi wa Wilaya yake kwa kuwakaribisha viongozi mbalimbali na kuzungumza nao masuala ya kiutumishi, jambo ambalo linawaongezea ari kubwa katika utendaji kazi wao kupitia utumishi wa umma.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi ameanza ziara ya kikazi jijini Dar es salaam yenye lengo kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa umma pamoja na kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kuzinusuru Kaya Maskini nchini unaoratibiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na watumishi wa Manispaa ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam (hawapo pichani), akiwa katika ziara yake ya kikazi yenye lengo la kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma walio katika Wilaya hiyo.
Sehemu ya Watumishi wa Umma wa Manispaa ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (hayupo pichani), alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa Wilaya hiyo.
Katibu Tawala wa Wilaya ya Kinondoni, Bi. Stella Msofe akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi kuzungumza na watumishi wa Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es salaam (hawapo pichani), wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma.
Mhandisi Mitambo wa Manispaa ya Kinondoni, Bw. Hamed Hamdun akiwasilisha hoja kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (hayupo pichani), wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es salaam.
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deogratius Ndejembi (katikati) akisikiliza hoja iliyokuwa ikiwasilishwa na mtumishi wa Manispaa ya Kinondoni, wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma wa Wilaya hiyo. Kulia kwake ni Katibu Tawala Wilaya ya Kinondoni, Bi. Stella Msofe na kushoto kwake ni Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kinondoni Mhe. Songoro Mnyonge.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Bi. Hanifa Suleiman akisoma taarifa fupi ya utekelezaji wa majukumu ya Manispaa ya Kinondoni kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deogratius Ndejembi wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma katika Wilaya ya Kinondoni.
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kinondoni Mhe. Songoro Mnyonge akitoa salamu za Manispaa ya Kinondoni kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deogratius Ndejembi wakati wa ziara ya Naibu Waziri huyo iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma katika Wilaya ya Kinondoni.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments