UPANGAJI SAFU KASULU UCHAGUZI MKUU 2025 WAMCHEFUA NAIBU KATIBU MKUU CCM


Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM Bara Christina Mndeme (aliyesimama katikati akizungumza na wajumbe wa halmashauri kuu ya CCM wilaya ya Kasulu akiwa kwenye ziara ya kichama mkoani Kigoma.
Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM Bara Christina Mndeme (aliyesimama katikati akizungumza na wajumbe wa halmashauri kuu ya CCM wilaya ya Kasulu akiwa kwenye ziara ya kichama mkoani Kigoma.
Wajumbe wa Halmashauri kuu ya CCM wilaya ya Kasulu, viongozi wa serikali wa wilaya hiyo na viongozi wa taasisi za serikali wilayani humo wakimsikiliza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara Christina Mndeme alipokuwa kwenye ziara ya kichama ya siku moja wilayani humo.
Katibu wa CCM mkoa Kigoma Mobutu Malima (aliyesimama kushoto) akizungumza mbele ya Naibu Katibu Mkuu wa CCM bara Christina Mndeme wakati wa kikao cha wajumbe wa halmashauri kuu ya CCM wilaya ya Kasulu ambacho kilikuwa maalum kwa ziara ya Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM bara ambaye yuko kwenye ziara ya kichama mkoani Kigoma.
Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM Bara Christina Mndeme (wa pili kushoto mstari wa mbele) akiwasili katika eneo la shule ya Sekondari Nkundutsi wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma ambapo alitembelea shule hiyo na baadaye kuzungumza na wanafunzi, walimu na jumuia ya shule hiyo akiwa kwenye ziara ya kichama mkoani Kigoma.(Picha na Fadhili Abdallah)
**

Na Fadhili Abdallah,Kigoma

UPANGAJI safu za ugombea ubunge na udiwani kwa uchaguzi wa mwaka 2025 umemchefua Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara Christina Mndeme ambapo amekemea mpango huo na kuwataka viongozi na wanachama wa CCM wilaya ya Kasulu wanaopanga mpango huo kuacha mara moja.

Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM Bara akizungumza na wajumbe wa halmashauri kuu ya CCM ya wilaya Kasulu alisema kuwa hali hiyo inachafua taswira nzuri nay a kuigwa ya CCM na kwamba watakaokaidi agizo la kuachana na mpango huo wataadhibiwa.

“Kuna shetani amewaingia hapa ambaye ameanza kuwavuruga ni lazime tukemee shetani huyo kwani pamoja na kuvuruga huku lakini pia anakivuruga chama na kuvuruga mipango ya Mwenyekiti wetu na Raisi wetu, hatutakubali,”Alisema Naibu Katibu Mkuu wa CCM.

Alisema kuwa amekuwa akipokea sifa mbaya ya viongozi na wanachama wa CCM kuhusu kupanga makundi ya nani wa kuchaguliwa na nani asichaguliwe kwenye uchaguzi mkuu mwaka 2025 hasa nafasi za wabunge na madiwani na vitendo vya rushwa na kudhalilishana vimekuwa vikitawala michakato hiyo.

Mpango huo unadaiwa kuyakumba majimbo ya Kasulu Mjini ambalo kwa sasa Mbunge wake ni waziri wa nchi ofisi ya waziri Mkuu kazi,ajira,vijana na watu wenye ulemavu, profesa Joyce Ndalichako na jimbo la Kasulu Vijijini ambalo mbunge wake ni Augustino Hole Vuma.

“Kasulu kuna watu wanapanga safu kwa ajili ya uchaguzi wa mwaka 2025 na hali hiyo imeanza kuleta shida na kuchafuana hatutakubali naomba mliache vinginevyo tutachukua hatua,mnapanga safu,mnatoa rushwa,mnachafuana mnafanya vibaya sana,”Alisema Mndeme.

Sambamba na hilo Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM alisema kuwa walioshindwa kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 wakubali matokeo na pia waungane na wenzao katika kujenga chama wakiendelea kuvuruga chama na viongozi wake tutachukua hatua.

Aidha aliwataka viongozi na wanachama kufanya chaguzi za chama zinazoendelea kwa kuzingatia kanuni za uchaguzi zinazotokana na katiba ya CCM ikiwemo kanuni za uongozi na maadili na kwamba ni lazima slogan ya chama inayosema kwamba chama kwanza mtu baadaye izingatiwe.

Naibu Katibu Mkuu bara alisema kuwa Wagombea ni lazima wazingatie miiko na maadili ya uongozi ambayo miongoni mwa vitendo vinavypigwa vita ni pamoja na utoaji na upokeaji wa rushwa, utoaji wa siri za vikao.

Kutoa siri za vikao kunatengeneza uadui baina yetu lakini siri hizo zinadhoofisha wagombea wetu katika chaguzi za nje ya chama au kuwapa nafasi wagombea ambao wana mapungufu.

Awali Katibu wa CCM mkoa Kigoma, Mobutu Malima alisema kuwa asilimia 90 ya viongozi wa chama wanaomaliza muda wao wamerudishwa na kupitishwa kugombea tena nafasi mbalimbali ndani ya chama hicho na kwamba vikao vimezingatia taarifa mbalimbali za matendo yao, nidhamu na yale waliyofanya kwenye chama.

Malima alisema kuwa Wapo wagombea ambao hawakupitishwa na vikao vya uchujaji wagombea vya chama hasa baada ya kujiridhisha kwamba makosa waliyokuwa wanatuhumiwa nayo yamethibitika ikiwemo usaliti ndani ya chama katika uchaguzi mkuu uliopita.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments