BASHUNGWA : RAIS SAMIA AMEFUNGUA NCHI NA KUSAIDIA ONGEZEKO LA UKUSANYAJI WA MAPATO

OR TAMISEMI
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Innocent Bashungwa amesema kumekuwa na ongezeko la ukusanyaji wa mapato katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kufuatia kufunguka kwa nchi na uwepo wa mazingira wezeshi ya kukuza uchumi nchini.


Ametoa kauli hiyo leo agosti 6, 2022 kwenye ziara ya Rais Samia ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya ampao amempongeza Mheshiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kufungua nchi.

Amesema kupitia takwimu za ukusanyaji wa mapato katika mwaka 2021/2022 Mkoa wa mbeya umekusanya kwa asilimia 105.


Amemuhakikishia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kuwa kwa kushirikiana na Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi watajipanga vyema kuhakikisha takwimu ya ukusanyaji wa mapato kwa asilimia 103 itakuwa ni kiwango cha kujipima hadi kufikia asilimia 150.


Ameendelea kufafanua kuwa Mkoa wa Mbeya ni mfano wa kuigwa kwa kutumia mapato ya ndani ambapo kwenye halmashauri saba kila Halmashauri imejenga kituo cha afya kimoja ikiwemo Halmashauri ya Chunya.


Ameendelea kufafanua kuwa Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 150 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba ambavyo vitasambazwa kwenye vituo vya afya na Hospitali za Wilaya ili miundombinu inayojengwa iweze kutoa huduma bora kwa jamii.


kuhusu ujenzi wa Hospitali ya Wilaya, Waziri bashungwa amesema katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali itatoa kiasi cha Shilingi milioni 900 kuanza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Chunya.


Akizungumzia kuhusu uhaba wa watumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Chunya amesema katika ajira mpya zilizotolewa, Serikali imepeleka waalimu 65 na wauguzi 26 ili kupunguza uhaba wa watumishi katika halmashauri hiyo.


Aidha, Kuhusu ujenzi wa miundombinu ya barabara kupitia TARURA amesema kuwa Serikali imeweza kuongeza bajeti kwa asilimia 185 ambapo kwa Halmashauri ya chunya walikuwa wanapata shilingi milioni 600 lakini katika bajeti ya 2022/2023 wametengewa shilingi bilioni 2.3 ili ujenzi wa miundombinu ya barabara.


Bashungwa amesema Ofisi ya Rais TAMISEMI itaendelea kushirikiana na wizara za kisekta kutatua kero za wananchi na haitakuwa kikwazo kusukuma miradi ya maendeleo ya nchi kwa wananchi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments