AUAWA KWA KUCHOMWA KISU AKIGOMBANIA MREMBO MPYA WA BAA

Wakaazi wa kijiji cha Motosiet eneo la Cherang’any kaunti ya Trans Nzoia walisalia katika mshangao baada ya kijana wa miaka 20 kudungwa kisu na rafikiye kwenye eneo la kuuza chang’aa hadi kufa.

Katika kisa cha Jumanne, Agosti 23,2022 mwendo wa saa nne usiku, Kevin Sakwa Wandabwa alidungwa kisu kifuani nje ya nyumba ya mfanyabiashara maarufu wa chang'aa Gladys Kipsingori.

 Sakwa na mshukiwa ambaye bado hajazuiliwa, inadaiwa walitofautiana kuhusu mrembo aliyeajiriwa na Kipsingori kuuza kinywaji hicho na wakati uo huo kuwatumbuiza walevi.


 "Ilitokea kwamba marehemu alimuona mmoja wa wasichana hao na kumwendea, lakini inaonekana rafiki yake mmoja alihisi wivu na kubishana naye katika ugomvi mkali," Chifu wa eneo Isaac Kichwen aliambia Nation.

Katika makabiliano hayo, mshukiwa alimchoma kisu Sakwa na kumwacha akivuja damu. Kamanda wa Polisi wa Kaunti hiyo, Jecinta Wesonga, alisema kisura huyo aliyekuwa akipiganiwa alitoroka huku wanakijiji waliokuwa na hasira wakichoma moto nyumba yake.

 Polisi pia wanamsaka Kipsingori, ambaye alitoroka baada ya kisa hicho, ili kurekodi taarifa yake. Mwili wa Sakwa ulipelekwa katika makafani hospitali ya Rufaa ya kaunti ya Kitale huku uchunguzi kuhusu tukio hilo ukiendelea.


 Kwingineko, mwanamke mmoja alivamia chumba cha kulala cha jirani yake huko Kibra, Nairobi na kumdunga kisu kwa madai ya kumpokonya mumewe. 


Akiwa mbele ya Hakimu Mwandamizi wa Mahakama ya Makadara Monica Maroro, Celestine Odipo alishtakiwa kwa kumpiga Rose Adhiambo.


 Katika kisa hicho kilichotokea Mei 30, Odipo aliambia mahakama kuwa alifika nyumbani kutoka kazini mwendo wa saa kumi jioni na kukuta nyumba yake ikiwa wazi.

Alisema alifikiri kwamba mtoto wake alikuwa ndani ya nyumba hiyo ndipo alipomkuta Adhiambo akiwa ameketi kitandani mwake.

 Bibi huyo aliyekasirika alimshutumu Adhiambo kwa kuiba mumewe. Walibishana kabla ya Odipo kumchoma kisu shingoni.

CHANZO - Tuko News

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments