MAKUMBUSHO YA TAIFA YAJA NA PROGRAM YA VIONJO VYA USWAHILI



Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa Dkt Noel Lwoga akizungumza na wanahabari katika majaribio ya program ya Vionjo vya Uswahili ambayo imefanyika katika Kijiji Cha Makumbusho jijini Dar es salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa Dkt Noel Lwoga akishiriki kula vyakula vya asili ambavyo vimeandaliwa Tamasha la majaribio ya program ya Vionjo vya Uswahili ambayo imefanyika katika Kijiji Cha Makumbusho jijini Dar es salaam.
Kaimu Mkurugenzi wa Kijiji Cha Makumbusho jijini Dar es salaam Mawazo Jamvi akiwaeleza wanahabari dhamira ya kuandaa Program hiyo Vionjo vya Uswahili ambayo imefanyika katika Kijiji hicho.
Mgeni Kutoka Vtah Amerika David Sreight akieleza anavyopendezwa na tamaduni za kitanzania.
Watalii ambao wamefika Katika Kijiji Cha Makumbusho Kwa ajili ya kujifunza tamaduni mbalimbali za mtanzania.
Baadhi ya watumbuizaji wa maadhi ya Vionjo vya kiswahili wakitumbuiza katika majaribio ya program ya Vionjo vya Uswahili ambayo imefanyika katika Kijiji Cha Makumbusho jijini Dar es salaam.(Picha na Mussa Khalid)

............................

NA MUSSA KHALID

Makumbusho ya Taifa jijini Dar es salaam imeanzisha program ya Vionjo vya Uswahili ili kuendeleza utalii wa Utamaduni wa Mtanzania kupitia Mila mbalimbali katika maeneo yao.

Akizungumzia program hiyo ambayo imefanyika Katika Kijiji Cha Makumbusho leo jijini Dar es salaam Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa Dkt Noel Lwoga amesema imelenga kugusa Watu wanaoishi Maisha ya uswahilini ikiwemo katika Mavazi,ngoma za asili Pamoja na vyakula.

Aidha Dkt Lwoga amesema kuwa program hiyo leo imefanyika kwa majaribio hivyo wanataraji kuizindua rasmi mwishoni mwa Mwezi wa tisa ambapo vitashiriki vikundi mbalimbali na hasa wenyeji wa mji huo.

"Program hii tunajaribu kuunganisha na Utalii hivyo tunategemea kuandaa Kwa kushikiana na hoteli za Dar es salaam Pindi wanapowaleta wageni pia waje Katika Kijiji Cha Makumbusho Kwa ajili ya kujionea Vionjo vya uswahilini"amesema Dkt Lwogwa

Dkt Lwoga ameyataja mambo matatu ambayo ndio dhamira ya kuziandaa program hizo kuwa ni Pamoja na kuhifadhi Utamaduni na Mila za mtanzania,Kutoa zao jipya katika utalii wa Utamaduni Kwa kuwakumbusha waepukane na Dhana ya kwamba mtalii ni mpaka aende mbugani kuangalia wanyama Pamoja na kuongeza mapato katika Taasisi hizo.

Kwa Upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Kijiji Cha Makumbusho jijini Dar es salaam Mawazo Jamvi amesema kuwa program hiyo baada ya kuizindua rasmi itakuwa ilifanyika kila Ijumaa ya mwisho wa Mwezi.

Jamvi amesema dhumuni la program hiyo hasa ni kuwafuata watu wote wanaokaa maeneo ya uswahilini badala ya kuwasubiri mpaka watembelee Kijiji Cha Makumbusho kwa kuwavutia na Vionjo vya uswahilini.

"Kwa Sasa hivi Kwa kuanzia tumeshirikisha vikundi vichache Mwananyamala, Manzese na wenyeji lakini pindi tutakapozindua tutashirikisha vikundi vingi lengo letu hasa ni kuhakikisha tunaudumisha zaidi utalii wa kiutamaduni"amesema Jamvi

Katika Program hiyo pia wameshiriki wadau mbalimbali wa Sanaa na mashindano yakiwemo ya Kuna Nazi ambapo Mzee Lukas ameibuka mshindi amesema amekuwa akishiriki mashindano hayo kila wakati kwani anahamasisha wakina baba kuendelea kuonyesha upendo Kwa kuwasaidia wake zao Nyumbani.

Naye Mgeni Kutoka Vtah Amerika David Sreight amesema wamekuwa wakifuatilia tamaduni za kitanzania kwani wamekuwa wakijifunza namna ya kuishi na tamaduni Hizo Katika Jamii zao hivyo ameipongeza Makumbusho Kwa kubuni matukio kama hayo.

Hata hivyo Imeelezwa kuwa kuanzishwa kwa program itakuwa ni moja ya zao jipya la utalii ili kutoa fursa kwa watalii wa ndani na nje kufurahia utamaduni wa Kitanzania.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments