BENKI YA NMB YAKUTANA NA KLABU YA BIASHARA KIGOMA...MAGESE ASEMA 'MAFUNZO YAMEWAJENGA WAFANYABIASHARA KWENYE MAFANIKIO'

Meneja wa kanda ya magharibi wa benki ya NMB Sospeter Magesse (aliyesimama kushoto) akitoa maelezo kwa wanachama wa klabu ya biashara ya benki hiyo wa wilaya ya Kasulu na Kibondo kuhusu matumizi ya simu na kadi za kielektorniki zinavyotumika kufanya miala na huduma za kifedha ikiwemo ya mikopo inayotolewa na benki ya NMB na manufaa ya huduma hiyo kwa wateja wakati wa kikao cha wanachama hao kilichofanyika wilayani Kasulu mkoani Kigoma mwishoni mwa wiki iliyopita. (Picha na Fadhili Abdallah).
Mkuu wa idara ya Biashara wa benki ya NMB makao makuu Alex Mgeni (kushoto) akizungumza na kutoa maelekezo mbalimbali ya namna ya kufanya biashara kwa ufanisi na kukabili changamoto za kibiashara wakati wa kikao na wanachama wa klabu ya biashara ya wateja wa benki hiyo wilayani Kasulu mkoani Kigoma.
Wanachama wa klabu ya biashara ambao ni wateja wa Benki ya NMB wilaya za Kasulu na Kibondo wakifuatilia mada zilizokuwa ikiwasilishwa katika mkutano wa wanachama hao uliofanyika wilayani Kasulu mkoani Kigoma mwishoni mwa wiki.
***

Na Fadhili Abdallah,Kigoma

BENKI ya NMB imesema kuwa semina na mafunzo yanayotolewa kwa wateja wa benki hiyo kupitia klabu za biashara za benki hiyo zimeleta mafanikio makubwa katika kuzingatia taratibu na miongozi ya huduma za kibenki nchini.

Meneja wa Kanda ya Magharibi wa benki ya NMB, Sospeter Magesse alisema hayo wakati wa kikao cha wanachama wa klabu ya biashara kutoka wilaya ya Kasulu na Kibondo kilichofanyika wilayani Kasulu.

Magesse alisema kuwa moja ya mambo ambayo yamesaidia wanachama wa vilabu hivyo ambao ni wateja wa benki ya NMB ni pamoja na kujua taarifa za huduma zinazotolewa na benki hiyo ikiwemo upatikanaji wa mikopo, taratibu za upatikanaji wa mikopo hiyo na namna ya kufanya marejesho kulingana na taratibu zilizowekwa.

Meneja huyo wa kanda ya Magharibi wa benki ya NMB alisema kuwa kufanyika kwa mikutano hiyo kumesaidia kuimarisha huduma za benki kwa maana ya kuongeza wateja, ongezeko kubwa la wateja wanaochukua mikopo lakini pia imepunguza changamoto kubwa zinazojitokeza baina ya wateja na benki hiyo.

Kwa upande wake Mkuu wa idara ya biashara wa benki ya NMB Makao makuu, Alex Mgeni alisema kuwa kufanyika kwa mikutano hiyo kupitia vilabu vya biashara vya benki hiyo vimewezesha wateja wa benki hiyo kuzifikia fursa mbalimbali zinazotolewa ikiwemo mikopo kwa ajili ya kuimarisha biashara zao na shughuli za kiuchumi.

Mgeni alisema kuwa zipo fursa nyingi za mikopo na huduma nyingine ambazo wafanyabiashara na wateja wa benki hiyo wanaweza kuzifikia ambazo hazijatumika kikamilifu na ambazo zinaweza kusaidia kuinua biashara na kuchangia kuongeza ukusanyaji wa mapato wa serikali.

Sambamba na hilo Mkuu wa kitengo cha Bima kutoka NBM Makao makuu, Martin Masawe aliwaasa wateja wa benki hiyo kuweka bima za biashara zao, majengo ya vitega uchumi, nyumba na vyombo vya o vya usafiri ili waweze kuondokana na hasara majanga yanapotokea.

Baadhi ya wanachama wa vilabu vya wafanyabiashara vya benki ya NMB waliohudhuria mkutano huo walisema kuwa mikutano hiyo imekuwa na manufaa makubwa kwao ikiwemo kujua namna ya kuchukua hatua kukabiliana na changamoto za kibiashara zinapojitokeza na urejeshaji mikopo.

Mmoja wa wateja hao Zaitun Buyogera alisema kuwa mikutano hiyo imewawezesha kukutana na wataalam wa masuala ya biashara sambamba na viongozi wa benki hiyo ambao wamewapa ufafanuzi wa mambo mengi ambayo yanawasaidia kuendesha biashara zao kwa ufanisi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments