UGONJWA ULIOLIPUKA LINDI NI 'HOMA YA MGUNDA' UNAAMBUKIZWA KUTOKA KWA WANYAMA KWENDA KWA BINADAMU


Waziri wa Afya Ummy Mwalimu
**
Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amesema kuwa upimaji wa sampuli za wagonjwa waliokuwa wakiugua Ugonjwa Usiojulikana katika Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi umethibitisha mlipuko huu kuwa ni ugonjwa wa Leptospirosis, ama Homa ya Mgunda.

Waziri Ummy amesema hayo leo mara baada ya kutembelea Wilaya ya Ruangwa katika Mkoa wa Lindi ambako kumezuka mlipuko wa ugonjwa huo na kuzungumza na waandishi wa habari ambapo amesema Homa ya Mgunda ni miongoni mwa magonjwa yanayoambukizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa Binadamu na unasababishwa na Bakteria aina ya Leptospira interrogans.

Ummy amesema “Ugonjwa huu umekuwepo katika maeneo ya kitropiki ambayo ni yenye hali ya joto katika mabara ya Amerika ya Kaskazini, Amerika ya Kusini, Afrika, Asia na Australia, wanyama aina za panya, kindi, mbweha, kulungu, swala, na wanyamapori wengine wameripotiwa kupata maambukizi ya vimelea hivi na kuwa chanzo cha maambukizi kwa Binadamu”

Amesema kuwa Ugonjwa wa Homa ya Mgunda huambukizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa Binadamu kupitia uchafuzi wa mazingira ikiwemo vyanzo vya maji kutoka katika mkojo wa wanyama wenye maambukizi.

Wizara inaendelea kuchukua hatua za kukabiliana na ugonjwa huu na kuendelea kutoa taarifa kwa umma kuhusu mwenendo wa ugonjwa huu. Hivyo Serikali inawaasa Wananchi kutokuwa na hofu kwani ugonjwa huu unaendelea kudhibitiwa” amesema Waziri Ummy Mwalimu.

Chanzo - Global Publishers

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments