MBUNGE MWIJAGE AZIPONGEZA OFISI NDOGO ZA TANESCO MULEBA


Waziri wa Nishati Mh. January Makamba akizungumza na wananchi wa Muutwe Muleba.
Viongozi  mbalimbali pamoja na wabunge wa Muleba Kaskazini na Kusini walioambatana na Waziri wa Nishati Januari Makamba katika ziara yake Muleba
Waziri wa Nishati Mh. January Makamba akimpongeza Mmiliki wa nyumba baada ya kuwasha umeme
Wa pili kulia ni Meneja Tanesco Mkoa wa Kagera Mhandisi Godlove Mathayo
Anayezungumza ni Meneja Tanesco Wilaya ya Muleba Injinia Lemk Said  na kulia kwake ni Meneja Tanesco Mkoa Mhandisi Godlove Mathayo


Na Mbuke Shilagi Kagera.

Mbunge wa Jimbo la Muleba Kaskazini Mh. Charles Mwijage amezipongeza ofisi ndogo za Tanesco zilizopo Izigo pamoja na Nshamba Muleba kwa kazi nzuri pamoja na juhudi wanazofanya kwa wananchi wake.

Ameyasema hayo jana Julai 17,2022 katika ziara ya siku tano ya Waziri wa Nishati Mh. January Makamba alipokutana na kuzungumza na wananchi wa Kata ya Muutwe Wilayani Muleba.

Mbunge Mwijage amesema kuwa utendaji kazi wa Tanesco kwa kuweka ofisi ndogo za Izgo na Nshamba umekuwa mzuri kwani wafanyakazi wake wamekuwa wakiwahudumia wananchi kwa wakati licha ya umbali unaokuwepo kutoka zilipo ofisi zao mpaka eneo la mteja.

Ameongeza kuwa ofisi hizo zimekuwa na eneo kubwa la utawala katika kazi ambapo linawapelekea kusafiri kwa mwendo mrefu kwa kutumia usafiri wa pikipiki ili kuwafikia wateja na kuwahudumia hivyo wapewe gari pale inapotakiwa.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Muleba Mh. Toba Nguvila amempongeza Waziri Makamba kwa kazi nzuri anazoendelea kufanya katika Nchi hasa Kagera ambapo ameweza kufanya ziara ya siku tano ili kutatua changamoto pamoja na kukagua Miradi inayoendelea.

"Unapokuwa na Waziri anapenda wananchi kama huyu January Makamba wananchi wanafurahi sana kwasababu unawatembelea na kutatua kero zao", amesema Mh. Nguvila.

Naye Waziri Makamba aliweza kuwasha umeme katika Kijiji cha Bukoki kitongoji cha Nshambya kata Muutwe pamoja na kugawa mitungi ya Ges kwa baadhi ya wananchi na kusema kuwa Mkoa wa Kagera ni muhimu sana na ni Mkoa wa kimkakati ambao upo mpakani hivyo unahitaji nishati.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments