MWENGE WA UHURU WAZINDUA MRADI WA MAJI BUGWANDEGE...SHUWASA YAPEWA TANO KUTUMIA VIZURI FEDHA ZA UVIKO - 19



Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Sahili Nyanzabara Geraruma akizindua Mradi wa Maji katika kijiji cha Bugwandege Manispaa ya Shinyanga, ambao umetekelezwa na Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA).

Ukaguzi Mradi wa Maji  ukiendelea katika Kijiji cha Bugwandege.

Na Marco Mduhu, SHINYANGA

KIONGOZI wa Mbio za Mwenge wa  Uhuru Kitaifa Sahili Nyanzabara Geraruma, amefungua  Mradi wa Maji katika kijiji cha Bugwandege Manispaa ya Shinyanga, ambao umewaondolea wananchi adha ya kutumia Maji Machafu.

Mradi  uliotekelezwa na SHUWASA  chini ya Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya Uviko -19 umefunguliwa  Julai 27, 2022.

Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Shinyanga (SHUWASA) Mhandisi Yusuph Katopola, amesema walipokea fedha za UVIKO-19 jumla ya Sh. milioni 469 kwa ajili ya kutekeleza Miradi mbalimbali ya Maji kwa Wananchi wa Bugwandege, Magwata, Bugimbagu, Didia na Iselamagazi  lakini wametumia Sh.milioni 406 na Miradi yote inatoa huduma ya Majisafi kwa wananchi, ukiwemo mradi huu  wa Bugwandege ambao utanufaisha wananchi 6,900 na kwa Maeneo yote idadi ya wanufaika ni 21,536.

Naye Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, amesema Mradi huo wa Maji safi na Salama umekuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi hao wa Bugwandege, ambao wameondokana na adha ya kutumia maji machafu pamoja na hofu ya Wanyama wakali kwa kufuata maji umbali mrefu.

“Tumpongeza Rais wetu Samia Suluhu Hassan, kwa kutuletea pesa hizi na kutekeleza miradi ya Maji safi na salama kwa wananchi na sasa mnakunywa Maji safi,”amesema Mboneko.

Aidha, Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini Patrobas Katambi, ambaye pia Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na wenye ulemavu, amesema kipindi cha kampeni cha uchaguzi mkuu mwaka 2020 waliahidi kupeleka Maji kijijini humo lakini sasa maji yapo na kumpongeza Rais Samia kuitekeleza ilani ya uchaguzi kwa vitendo.

Kwa upande wake kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2022 Sahili Nyanzabara Geraruma, ameupongeza Mradi huo na kutoa msemo kuwa popote mama alipo Maji yamemfikia na kumtua ndoo kichwani.

Pia ametoa wito kwa wananchi wa kijiji hicho cha Bugwandege kuitunza miundombinu ya mradi huo wa maji, pamoja na kuvuta maji majumbani mwao na kuacha kuchota kwenye vituo vya kuchotea maji.

Mwenge wa Uhuru upo mkoani Shinyanga, na leo umekimbizwa katika Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, ambapo kesho utakimbizwa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu.

Kauli Mbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka huu (2022) inasema "Sensa ni Msingi wa Mipango ya Maendeleo, Shiriki kuhesabiwa kwa Maendeleo ya Taifa.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Sahili Nyanzabara Geraruma, akizungumza alipofika kuzindua Mradi wa Maji safi na Salama katika Kijiji cha Bugwandege Manispaa ya Shinyanga, uliotekelezwa na (SHUWASA).
Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini Patrobas Katambi, ambaye pia Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na wenye ulemavu, akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mradi wa Maji kijiji cha Bugwandege.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akizungumza kwenye uzinduzi wa Mradi wa Maji kijiji cha Bugwandege.

Mkurugenzi Mtendaji wa (SHUWASA) Mhandisi Yusuph Katopola, akitoa taarifa ya utekelezaji wa Mradi wa Maji katika kijiji cha Bugwandege na miradi mingine ambayo inatokana na fedha za UVIKO-19.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Sahili Nyanzabara Geraruma, (kulia) akizungumza na Mkurugenzi wa (SHUWASA) Mhandisi Yusuph Katopola.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Sahili Nyanzabara Geraruma akizundua Mradi wa Maji katika kijiji cha Bugwandege Manispaa ya Shinyanga, ambao umetekelezwa na Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA).

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Sahili Nyanzabara Geraruma, akimtwisha Ndoo ya Maji Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini Patrobas Katambi, ambaye pia ni Naibu Waziri Ofsi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na wenye ulemavu, mara baada ya kumalizi kuzindua Mradi wa Maji katika Kijiji cha Bugwandege.

Wajumbe wa Bodi Mamlaka ya Maji Shinyanga (SHUWASA) wakishuhudia uzinduzi wa Mradi wa Maji katika Kijiji cha Bugwandege-Ibadakuli Manispaa ya Shinyanga.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments