CWT YAWAKUMBUSHA WALIMU UMUHIMU WA KUJIUNGA NA MFUKO WA HIFADHI YA JAMII


Mwenyekiti wa Chama cha Walimu (CWT) wilaya ya Bariadi Mkoani Simiyu Magambo Petro akifungua semina ya siku moja ya Walimu wilayani humo iliyoandaliwa na CWT.

Na COSTANTINE MATHIAS, Bariadi.

CHAMA Cha Walimu (CWT) Mkoa wa Simiyu kimewataka Walimu Wilayani Bariadi kuhakikisha wanajiunga na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii ili iweze kuwasaidia na kuwanufaisha mara baada ya kustaafu Utumishi wa Umma.

Hayo yamebainishwa leo na Katibu wa CWT Mkoa wa Simiyu Ponsian Gervas kwenye Semina ya siku moja iliyowakutanisha walimu wa Halmashauri ya wilaya na Mji wa Bariadi iliyofanyika katika ukumbi wa Kusekwa Memoarial Sekondari, semina ambayo imewashirikisha walimu wa shule za Msingi, Sekondari pamoja na waratibu Elimu Kata.

Gervas alisema mwaka 2019 sheria ilitunga kwamba kila mtumishi atachangia asilimia 5 ya mshahara wake huku mwajiri akiongeza asilimi 15 ya mshahara wa mwalimu husika.

"Asilimia 20 ya mshahara wako inakwenda kila mwezi, inatunza au inawekwa kwenye uwekezaji kwenye mfuko ambao unalipa mafao au kiinua mgongo kwa mfanyakazi au mtumishi wa umma akistaafu’’ alisema Gervas.

Alifafanua kuwa anayelipa kiinua mgongo au mafao ni Mfuko wa hifadhi ya Jamii na kwamba mtumishi atalipwa kulingana na alivyochangia michango yake ya asilimia 5 pamoja na asilimia 15 za mwajiri wake.

"Kuna watu hawachangii au hawakatwi, wanasema wanasevu, mwisho wa siku, siku ya kustaafu kwako utatoka kama ulivyoingia hautapata hata senti tano…kama kuna mtu wa namna hii, baada ya kikao hiki akajisalimishe kesho asubuhi’’ alisema Gervas.

Aliongeza kuwa Mtumishi anapochangia mfuko wa hifadhi ya Jamii na bahati mbaya akafariki dunia akiwa ametimiza vigezo au sifa vya kuchangia kwa muda wa miezi miaka 15 au miezi 180.

Na kwamba, Mfuko utamlipa kiinua mgongo na pensheni mwenzi au mjane aliyeaachwa kwa maisha yake yote na kwamba akiolewa au kuoa anakuwa hana sifa za kuendelea kulipwa.

Awali akifungua Semina hiyo, Mwenyekiti wa CWT wilaya ya Bariadi Magambo Petro alisema CWT iko mstari wa mbele kuhakikisha haki na maslahi ya walimu yanapatikana licha ya walimu kuzungukwa na changamoto mbalimbali.

Alisema suluhisho pekee la Walimu kutatua changamoto zao ni Chama cha Walimu, ambapo hadi sasa kati ya kesi 36 zilizofika ofisini, ni kesi moja tu inaendelea kushughulikiwa huku zingine zote zimeshatatuliwa.

"Kuna wakati unaweza kukiona katika mtizamo hasi, chama cha dhuluma… lakini kuna wakati walimu mlithibitisha kuwa chama kipo kwa maslahi ya Walimu, kama unachangamoto zinazokukabiliwa Mwalimu na uko CWT, tambua uko sehemu sahihi’’ alisema Petro.

Akiwasilisha Historia ya Chama Cha Walimu, Asha Juma ambaye ni Katibu wa CWT wilaya ya Busega alisema walimu wengi wameshindwa kutofautisha kati ya Chama cha Wafanyakazi na Mwajiri au chama cha kutoa mafao na chama cha wafanya kazi.

Aliwataka walimu hao kutofautisha vyama hivyo ambapo kila chama kimeundwa kwa mujibu wa sheria na kanuni zake, ambapo aliwata walimu kuvitumia vizuri vyama hivyo ili viweze kuwanufaisha pamoja na kupata stahiki na madai yao.
Mwenyekiti wa Chama cha Walimu (CWT) wilaya ya Bariadi Mkoani Simiyu Magambo Petro akifungua semina ya siku moja ya Walimu wilayani humo iliyoandaliwa na CWT.
Katibu wa Chama cha Walimu (CWT) mkoa wa Simiyu Ponsian Gervas akiongea na Walimu (hawapo pichani)
Mratibu Elimu kata ya Mhango Julian Mbakiza akiwasilisha salam toka za Maafisa Elimu kata, kwenye kikao cha Walimu kilichofanyika ukumbi wa Kusekwa Memoria Sekondari mjini Bariadi.
Asha Juma, Katibu wa CWT wilaya ya Busega mkoani Simiyu akitoa maada kwa Walimu leo


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments