WANAWAKE WA OSHA WAWAFARIJI WAGONJWA MOI, MUHIMBILI

Jumuiya ya wakina mama wa OSHA wakiwa katika jengo la Taasisi ya Mifupa ya Moi walipotembelea Taasisi hiyo kwa lengo la kutoa vifaa pamoja na mahitaji mbalimbali kwa wakina mama waliojifungua watoto wenye changamoto za mgongo wazi na vichwa vikubwa pamoja na wodi ya wazazi katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Baadhi ya wanawake wa OSHA wakitoa faraja kwa mzazi aliyejifungua mtoto mwenye changamoto ya mgongo wazi walipotembelea wodi ya wazai hao katika Taasisi ya Mifupa ya MOI.


Mwakilishi wa Jumuiya ya wakina mama wa OSHA Amina Nangu akikabidhi baadhi ya vifaa kwa muuguzi anayehudumia katika wodi ya wakina mama wanaojifungua watoto wenye changamoto ya vichwa vikubwa na migongo wazi walipotembelea wodi hiyo kwa lengo la kutoa faraja kwa wazazi hao.

Wawakilishi wa Jumuiya ya akina mama wa OSHA wakipokelewa vifaa mbali mbali walivyoviandaa kwa ajili ya kutoa msaada kwa akina mama wanaojifungua watoto wenye changamoto ya vichwa vikubwa na migongo wazi katika Taasisi ya Mifupa ya MOI.

************

Na Mwandishi Wetu

Jumuiya ya wafanyakazi wanawake wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) wamefanya ziara katika Taasisi ya Mifupi ya Moi kwa lengo la kuwafariji na kuwapa mahitaji muhimu watoto waliozaliwa na changamoto za migogo wazi na vichwa vikubwa ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani.

Akina mama hao kutoka OSHA wametembelea wodi la watoto wenye migogo wazi na vichwa vikubwa katika Taasisi ya Mifupa ya MOI pamoja wodi la wazazi katika Hospitali ya Taifa ya Muhumbili ambapo wametoa msaada wa mahitaji mbali mbali muhimu.

Akimwakilisha Mtendaji Mkuu, Bi. Khadija Mwenda, katika ziara hiyo, Mkaguzi wa Afya wa OSHA, Bi. Amina Nangu, amesema Taasisi ya OSHA imekuwa na desturi ya kusaidia makundi mbali mbali katika jamii yenye mahitaji maalum.

“Tumewawakilisha akina mama wenzetu kuja mahali hapa kwa ajili ya kuwafariji akina mama ambao wanawauguza watoto wao waliozaliwa wakiwa na changamoto ya vichwa vikubwa na migongo wazi. Tunatambua kwamba wana changamoto nyingi na wanahitaji sana misaada ya hali na mali kutoka kwa watu mbali mbali hivyo tunaomba wapokee kidogo tulichokuja nacho kama ishara ya upendo wetu kwao na tunawasihi wasijione wapweke na watambue kwamba tuko pamoja nao,” amesema Amina Nangu, Mkaguzi wa Afya wa OSHA.

Maafisa Ustawi wa Jamii wa MOI wamewashukuru wanawake kutoka OSHA kwa kusaidia kutatua baadhi ya changamoto za wagonjwa hao sambamba na kutoa wito kwa wanajamii wengine kuguswa na changamoto za wagonjwa hao hususan watoto wenye migogo wazi na vichwa vikubwa ambazo walieleza kuwa ni nyingi kutokana na kutakiwa kukaa hospitalini hapo kwa muda mrefu.

Aidha, waliwaomba wanawake hao kutoka OSHA kuwa mabalozi katika jamii kuhusiana na changamoto hiyo ya watoto kuzaliwa na vichwa vikubwa na migongo wazi ambapo walielezwa kwamba linatokana na ukosefu wa vitamini B9 (folic acid) miongoni mwa akina mama wajawazito.

“Nawashukuru sana akina mama wa OSHA kwa kuwatembelea hawa akina mama wenye watoto wenye vichwa vikubwa na migongo wazi na natumai kuwa mtakwenda kuwa mabalozi wazuri katika jamii yetu kuhusiana na namna sahihi ya kuondokana na tatizo hili,amesema Theresia Jacob ambaye ni Afisa Maendeleo ya Jamii-MOI.

Kwa upande wao, wagonjwa waliotembelewa na kufarijiwa na wanawake kutoka OSHA akiwemo Erica Johanes wamewashukuru wanawake wenzao kutoka OSHA ambapo wamesema wanawaombea Baraka kutoka kwa mwenyezi Mungu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments