TANZANIA KUWA MWENYEJI WA MKUTANO KUKABILIANA NA UJANGILI BARANI AFRIKA


Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) akitoa shukrani kwa niaba ya Mawaziri wa nchi wanachama wa Mkataba wa Lusaka kuhusu kukabiliana na ujangili na usafirishaji haramu wa mazao ya wanyamapori na mimea katika kikao cha mkutano wa 13 wa Baraza la Uongozi la Mkataba wa Lusaka kilichofanyika leo Livingstone, ZambiaNaibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) (kulia) akitia saini maazimio ya Baraza la Uongozi la Wanachama wa mkutano wa 13 wa Mkataba wa Lusaka katika kikao kilichofanyika leo Livingstone, Zambia. Kushoto ni Rais wa Mkutano wa 12 wa Baraza Tawala la Nchi Wanachama wa Mkataba wa Lusaka na Waziri wa Maliasili na Utalii wa Zambia, Mhe. Rodney Sikumba (Mb) akitia saini maazimio hayo.Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) (wa saba kutoka kushoto) katika picha ya pamoja na Mawaziri na Sekretarieti kutoka nchi wanachama wa mkutano wa 13 wa Baraza la Uongozi la Mkataba wa Lusaka mara baada ya kikao kilichofanyika leo Livingstone, Zambia. 

Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Zambia, Mhe. Hassan Simba Yahya (katikati) akifuatilia mada wakati wa mkutano wa 13 wa Baraza la Uongozi la Mkataba wa Lusaka kuhusu kukabiliana na ujangili na usafirishaji haramu wa mazao ya wanyamapori na mimea, kilichofanyika leo Livingstone, Zambia. 

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) (katikati), Rais wa Mkutano wa 12 wa Baraza Tawala la Nchi Wanachama wa Mkataba wa Lusaka na Waziri wa Maliasili na Utalii wa Zambia, Mhe. Rodney Sikumba (Mb)(kushoto) na Balozi wa Japan nchini Zambia, Mhe. Ryuta Mizuuchi wakiwa wamesimama ulipopigwa wimbo wa Taifa wa Zambia wakati wa mkutano wa 13 wa Baraza la Uongozi la Mkataba wa Lusaka uliofanyika leo Livingstone, Zambia. 

************************ 

Tanzania inatarajia kuwa mwenyeji wa mkutano wa kukabiliana na ujangili na usafirishaji haramu wa mazao ya wanyamapori na mimea ndani na nje ya Bara la Afrika. 

Hayo yamesemwa leo na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) wakati wa hitimisho la mkutano wa 13 wa Baraza la Uongozi la Mkataba wa Lusaka(The 13rd Governing Council of the Lusaka Agreement) katika kukabiliana na ujangili na usafirishaji haramu wa mazao ya wanyamapori na mimea ndani na nje ya Bara la Afrika uliofanyika jijini Livingston nchini Zambia. 

“Nchi itafaidika na mkutano huo kwa sababu tumekuwa na changamoto kubwa ya mapambano dhidi ya maharamia wanaodhuru wanyama wetu na hivyo tutakomesha biashara haramu.” Mhe. Masanja amefafanua. 

Amesema mkutano huo utafanyika mwezi Mei mwaka 2024 na unatarajiwa kuwa na washiriki zaidi ya 100 na utakuwa na manufaa makubwa kwa Tanzania kwa sababu kuna mashirika mbalimbali ambayo yanayojitokeza kuzisaidia nchi za Afrika ambazo zinapambana na ujangili wa misitu na wanyamapori. 

Ameongeza kuwa kama Tanzania itafikia masharti yaliyowekwa, kitajengwa kituo cha kupambana na ujangili wa misitu na wanyamapori jijini Arusha lengo ni kudhibiti ujangili wa misitu na wanyamapori na kuhakikisha biashara haramu ya ujangili wa wanyamapori na misitu inakomeshwa. 

Akiongelea kuhusu Mkataba wa Lusaka, Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Zambia, Mhe.Hassan Simba Yahya amesema mkataba huo unajihusisha na kuzuia uuzaji, usafirishaji wa wanyamapori pamoja na mimea hivyo utasaidia katika kupambana na ujangili na uhamishaji wa wanyama na mimea ambayo iko katika hatari za kutoweka. 

Amesema Tanzania imeshiriki katika mkutano wa 13 wa Baraza la Uongozi la Mkataba wa Lusaka katika kukabiliana na ujangili na usafirishaji haramu wa mazao ya wanyamapori na mimea ndani na nje ya Bara la Afrika ambao maamuzi yake yatainufaisha Tanzania kama nchi mwanachama. 

Mkutano huo umehudhuriwa na Mawaziri Wanachama kutoka nchi za Congo, Lesotho, Liberia, Tanzania, Uganda na Zambia. Nchi zingine zilishiriki kama Waangalizi (Observers) ni Niger, Senegal, Angola, Malawi, Mozambique, Togo, Ivory Coast, Benin, Ghana, Guinea , Burkina Faso na Nigeria.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments