DC MBONEKO AIPONGEZA LIFEWATER KUTEKELEZA KIKAMILIFU MRADI WA MAJI NA USAFI WA MAZINGIRA MWANTINI

 

Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akinawa mikono kwenye Kituo cha kunawia mikono katika shule ya Msingi Bushoma kata ya Mwantini kilichojengwa na Shirika la LifeWater International.

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko amelipongeza Shirika la Kimataifa la LifeWater International kwa kushirikiana na Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) kutekeleza kikamilifu Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira katika vijiji vya Bushoma na Mishepo kata ya Mwantini,kujenga vyoo na vituo vya kunawia mikono kwenye shule za msingi Jimondoli,Bushoma na Ng’hama zilizopo katika halmashauri ya Shinyanga.

Mboneko ametoa pongezi hizo leo Jumatano Machi 16,2022 alipotembelea miradi ya maji katika kata ya Mwantini halmashauri ya wilaya ya Shinyanga ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Maji nchini Tanzania.

“Tupo kwenye Wiki ya Maji na kwenye wiki hii ya maji tunapitia, kukagua na kuangalia utekelezaji wa maelekezo ya serikali kwenye upande wa maji,kuna maeneo mheshimiwa Rais ameleta fedha kwa ajili ya kukamilisha miradi lakini pia kuna maeneo wadau wetu wa maendeleo katika sekta ya maji na wenyewe pia wameshirikiana na sisi kwa hiyo ndiyo tupo kwenye mchakato huo”,amesema Mboneko.

“Tunayo furaha kubwa wadau wetu wazuri LifeWater International mmeshirikiana na serikali yetu na upande wa RUWASA kuhakikisha kuwa maji eneo la Mwantini (Mishepo na Bushoma) wanapata maji, hongereni sana na tunawashukuru sana LifeWater. Haya maji tumeyapima ni maji salama, bora kwa kunywa na kuoga na tutaendelea kuyapima mara kwa mara”,amesema Mboneko.

Amesema kukamilika kwa mradi huo sasa kutaondoa changamoto ya upatikanaji wa maji katika maeneo ya Bushoma na Mishepo kwa sababu ilikuwa ni kero ya muda mrefu.

“Wakati LifeWater walipokuja ofisini kwangu kujitambulisha na kunieleza kuhusu mradi huu,niliwapa maelekezo. Niliwaambia mkitaka mfanikiwe shirikisheni uongozi wa kwenye kata husika wote, waelewe mradi na watawapa ushirikiano asilimia 100 na nikasema viongozi wote waliopo kwenye ngazi ya serikali, watendaji na wenyewe watoe ushirikiano mtapata mkishirikiana na maafisa tarafa. Ninayo furaha kuona yale niliyowaelekeza wameyafanya. Mradi huu umeenda kama tulivyotarajia”,amesema Mboneko.

Amewataka RUWASA na LifeWater kuendelea kuelimisha wananchi kutunza chanzo cha maji wasifanye shughuli za kilimo ili kiwe endelevu sambamba na kutunza miundombinu ya maji pamoja na Kamati za maji zisimamie mapato vizuri.

“Tunawashukuru LifeWater kwa kujenga vyoo katika shule tatu na kuweka sehemu za kunawia mikono za kisasa kabisa. Mradi huu umekuwa wa mafanikio makubwa sana.Watoto wetu wanatumia vyoo bora na maji safi wanayatumia ili wasipate magonjwa mbalimbali. Mmeleta furaha katika jamii yetu”,amesema.

“Natumia fursa hii kuwapongeza viongozi wa kata ya Mwantini kwa kusimamia wananchi kushiriki katika mradi kwa kuchimba mitari ili maji yafike kwao, wameokoa shilingi milioni 24”,ameongeza Mboneko.

Naye Diwani wa kata ya Mwantini, Mpemba Jilungu na Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Shinyanga Vijijini, Edward Ngelela wamelishukuru Shirika la LifeWater kwa kushirikiana na RUWASA kuwapatia mradi huo na kwamba wameahidi kuutunza ili uwe endelevu.

Akitoa taarifa kuhusu Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira kata ya Mwantini, Mkurugenzi wa Shirika la LifeWater International, Devocatus Kamara amesema hivi sasa Mkoani Shinyanga wanatekeleza mradi wake wa kwanza wa miaka mitatu kuanzia mwaka 2021 hadi 2023 katika kata za Mwantini, Mwalukwa na Mwamala katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.

“Ukarabati na upanuzi wa mradi wa maji ya kisima kirefu Mishepo ulihusisha ufungaji wa Solar Pump mpya na mifumo yake, kutandaza mabomba mapya ya maji kutoka chanzo mpaka kwenye tenki la maji na kupanua mtandao wa maji katika kijiji cha Bushoma (kaya 513) kwa kujenga gati 5. Gati 11 za zamani zilikarabatiwa hivyo kuwezesha mtandao wote kuwa na gati 16 zinazofanya kazi zikihudumia wakazi 4,200”,ameeleza Kamara.

“Kukamilika kwa mradi huu kuligharimu jumla ya shilingi za Kitanzania 256,569,000/= ikijumlisha mchango wa jamii ambayo ilichangia kwa kuchimba na kufukia mtaro wa maji urefu wa kilomita 7.36 ambao unakadiriwa kugharimu shilingi 24,000,000/=. Kwa kushirikiana na RUWASA tumeweza kutoa mafunzo kwa kamati 8 za maji na tumetoa mafunzo na vitendea kazi kwa wahudumu wa kujitolea 184 ambao wanaendelea kutoa elimu ya usafi wa mazingira”,ameongeza.

Katika hatua nyingine amesema LifeWater International imefanikiwa kukarabati vyoo vine vyenye jumla ya matundu 29 katika shule za msingi Kilimawe na Hinduki (kata ya Mwantini) na Bunonga (kata ya Mwamala) pamoja na kujenga vituo vya kunawia mikono mashuleni katika shule za msingi Jimondoli, Bushoma na Ng’hama samba na kukamilisha ujenzi wa vyoo vipya vine katika shule za msingi Hinduki,Bunonga na Ng’hama vyenye jumla ya matundu 21.


“LifeWater International tunajishughulisha na uhamasishaji jamii na kushirikiana na serikali kujenga miundombinu vijijini kwa lengo la kuboresha huduma za maji safi na usafi wa mazingira likilenga jamii, shule za msingi na taasisi za huduma ya afya zilizopo vijijini. Huwa tunatekeleza shughuli zetu kwa kushirikiana na viongozi na wataalamu wa serikali katika ngazi husika”,ameongeza Kamara.

ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Mkurugenzi wa Shirika la LifeWater International, Devocatus Kamara akiwa katika Gati la maji kijiji cha Mishepo akimwelezea Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko (katikati) kuhusu Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira katika vijiji vya Bushoma na Mishepo kata ya Mwantini halmashauri ya wilaya ya Shinyanga. Kulia ni Meneja Miradi wa LifeWater International mkoa wa Shinyanga, Benety Malima. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Kulia ni Mkurugenzi wa Shirika la LifeWater International, Devocatus Kamara akiwa katika Gati la maji kijiji cha Mishepo akimwelezea Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko (katikati) kuhusu Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira katika vijiji vya Bushoma na Mishepo kata ya Mwantini halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akinawa mikono kwenye Kituo cha Kunawia mikono katika shule ya Msingi Bushoma kata ya Mwantini kilichojengwa na Shirika la LifeWater International. Vituo vingine vimejengwa katika shule ya Msingi Jimondoli na Ng'hama katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Mkurugenzi wa Shirika la LifeWater International, Devocatus Kamara (katikati) akimwelezea Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko kuhusu Kituo cha kunawia mikono katika shule ya Msingi Bushoma kata ya Mwantini kilichojengwa na Shirika la LifeWater International.
Wanafunzi wakinawa mikono kwenye kituo cha kunawia mikono katika shule ya Msingi Bushoma kata ya Mwantini kilichojengwa na Shirika la LifeWater International.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko (kulia) akiangalia Wanafunzi wakinawa mikono kwenye kituo cha kunawia mikono katika shule ya Msingi Bushoma kata ya Mwantini kilichojengwa na Shirika la LifeWater International.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza baada ya kukagua Kituo cha Kunawia mikono katika shule ya Msingi Bushoma kata ya Mwantini kilichojengwa na Shirika la LifeWater International. Vituo vingine vimejengwa katika shule ya Msingi Jimondoli na Ng'hama katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Muonekano upande wa pili wa Kituo cha Kunawia mikono katika shule ya Msingi Bushoma kata ya Mwantini kilichojengwa na Shirika la LifeWater International. Kituo hicho kina sehemu 12 za kunawia mikono
Kaimu Meneja wa RUWASA wilaya ya Shinyanga, Mhandisi Emael Nkopi akielezea namna wanavyoshirikiana na Shirika la LifeWater International kutekeleza miradi ya maji na usafi wa mazingira
Mkurugenzi wa Shirika la LifeWater International, Devocatus Kamara akiwashukuru viongozi na watalaamu mbalimbali kwa ushirikiano wanaotoa katika kutekeleza miradi ya maji na usafi wa mazingira
Mkurugenzi wa Shirika la LifeWater International, Devocatus Kamara akimshukuru Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko ,viongozi na watalaamu mbalimbali kwa ushirikiano wanaotoa katika kutekeleza miradi ya maji na usafi wa mazingira
Diwani wa kata ya Mwantini, Mpemba Jilungu akilishukuru Shirika la LifeWater kwa kushirikiana na RUWASA kuwapatia mradi wa maji.
Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Shinyanga Vijijini, Edward Ngelela akilishukuru Shirika la LifeWater kwa kushirikiana na RUWASA kuwapatia mradi wa maji.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza baada ya kutembelea Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira katika vijiji vya Bushoma na Mishepo kata ya Mwantini halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza baada ya kutembelea Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira katika vijiji vya Bushoma na Mishepo kata ya Mwantini halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza baada ya kutembelea Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira katika vijiji vya Bushoma na Mishepo kata ya Mwantini halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akipiga ya kumbukumbu na wadau wa maji na usafi wa mazingira baada ya kutembelea Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira katika vijiji vya Bushoma na Mishepo kata ya Mwantini halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akipiga ya kumbukumbu na wadau wa maji na usafi wa mazingira baada ya kutembelea Mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira katika vijiji vya Bushoma na Mishepo kata ya Mwantini halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.


Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Soma pia :

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments