UWT MKOA WA NJOMBE WAFANIKIWA KUSHIKA NAFASI YA TATU USIMAMIZI WA MIRADI YA KIUCHUMI


******************

UMOJA wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi (UWT)Mkoa wa Njombe umefanikiwa kushika nafasi ya tatu katika usimamizi wa miradi ya kiuchumi ya Chama hicho huku ukiahidi kuongeza kasi hiyo kwa ajili ya matokeo bora zaidi.

Akizungumza muda mfupi mara baada ya kukabidhiwa cheti za pongezi kutokana na ushindi huo kutoka kwa Katibu Mkuu wa CCM Daniel Chongolo, katika Kikao cha kawaida cha Baraza Kuu la UWT Taifa kilichofanyika Jijini Dodoma,

Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Njombe Scholastika Kevela alisema wao kama wanawake wa Chama cha Mapinduzi wa mkoa huo, wamekoshwa na ushindi huo kwa kuwa umeonyesha kuwa mchango wao katika usimamizi wa miradi wa kiuchumi ya chama unaonekana.

"Sisi kama wanawake wa UWT wa Njombe tumefarijika sana na ushindi huu na zaidi umetupa chachu ya kuendelea kuhakikisha tunaongeza usimamizi wa miradi hiyo kwa ajili ya matokeo chanya ndani ya chama chetu" alisema Mama Kevela

Aidha alisema malengo ya Umoja huo ni kuendelea kushirikiana kwa pamoja na kuweka mkazo katika usimamizi wa miradi hiyo na mingine ya kimaendeleo inayotekelezwa na chama hicho kama moja ya majukumu yake.

Alisema usimamizi mzuri katika miradi hiyo ndiyo njia pekee itakayokiwezesha chama hicho kupiga hatua mbalimbali za maendeleo kutokana na umuhimu wake katika kuchangia mapato ya chama hicho.

Nafasi ya kwanza katika eneo la usimamizi wa miradi hiyo imechukuliwa na Mkoa wa Arusha, na na Mkoa wa Mwanza ukichukia nafasi ya pili huku yote ikipewa cheti cha pongezi kwa hatua hiyo.

UWT mkoa wa Njombe pia imeushukuru uongozi wa UWT Taifa kwa kutambua juhudi wanazozifanya na kutambua mchango wao huku ikiahidi kuendelea kutoa ushirikiano wa kutosha katika kukikuza chama hicho.

Katika hatua nyingine Mwenyekiti huyo wa UWT mkoa wa Njombe amepongeza juhudi mbalimbali zinazofanywa na Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais Samia Suluhu Hassan kulitumikia Taifa.

" Tupo naye na tutaaendelea kumuunga mkono kwa vitendo katika harakati zake za ujenzi wa Taifa tukizidi kusisitiza kuwa kazi iendelee kama anavyosisitiza" aliongeza Mwenyekiti huyo wa UWT Mkoa wa Njombe Scholastika Kevela.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments