RAIS MSTAAFU KIKWETE AONGOZA HARAMBEE UJENZI WA OFISI ZA TAWLA DODOMA


Rais Mstaafu wa wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Kikwete (kushoto) akipokea Tuzo kutoka kwa Makamu Mwenyekiti wa TAWLA Stella Rweikiza (kulia) katika harambee iliyolenga kukusanya fedha kwaajili ya kumalizia ujenzi wa jengo la Chama hicho Jijini Dodoma. Harambee hiyo ilifanyika Disemba 3, 2021 katika hoteli ya Serena Dar es Salaam.
Makamu Mwenyekiti wa TAWLA Stella Rweikiza (wa pili kulia) akimkabidhi Tuzo Rais Mstaafu Dkt. jakaya Kikwete (wa pili kushoto) katika hafla hiyo, (wa kwanza kushoto), ni Mkurugenzi Mtendaji wa TAWLA Tike Mwambipile.


Rais Mstaafu wa wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Kikwete akizungumza na Wanachama wa TAWLA na wadau mbalimbali wa Sheria walioudhuria hafla hiyo.

Wakili Mary Richard ambaye pia ni mwanachama wa TAWLA akizungumza kwenye hafla hiyo kuelezea mafanikio ya Chama hicho katika kipindi cha miaka kumi mpaka sasa.
Mmoja wa waanzilishi wa TAWLA Balozi Mwanaidi Maaja akizungumza kwenye hafla hiyo akielezea historia ya Chama hicho, changamoto walizopitia na mafanikio waliyopata.




Wanachama wa TAWLA walioshiriki hafla hiyo wakifuatilia hotuba mbalimbali za viongozi.
Wageni waalikwa na wadau wa Sheria wakisikiliza hotuba ya Mgeni rasmi Dkt. Jakaya Kikwete (hayupo pichani) kwenye hafla hiyo.

Mkurugenzi Mtendaji wa TAWLA Tike Mwambipile akizungumza kwenye harambee hiyo akielezea namna ambavyo walivyoanza ujenzi wa Ofisi za Taasisi hiyo na hatua iliyofikia.
Rais mstaafu wa awamu ya Nne Mhe. Dkt. Jakaya Kikwete akifuatilia maelezo ya Mkurugenzi wa TAWLA Tike Mwambipie (hayumo pichani) wakati wa harambee hiyo.
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete (wa tatu kulia) akiwa na Makamu Mwenyekiti wa TAWLA Stella Rweikiza (wa pili kulia), pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Tike Mwambipile (kushoto) katika harambee hiyo iliyofanyika Disemba 3,2021 kwenye hotel ya Serena Jijini Dar es Salaam. (PICHA NA HUGHES DUGILO)




********************

Na: Hughes Dugilo, DAR ES SALAAM.
Imeealezwa kuwa licha ya kuwepo kwa mwamko mkubwa wa wanawake kutafuta msaada wa kisheria wanapopatwa na changamoto mbalimbali katika jamii lakini bado lipo tatizo kubwa la kuchelewa kutoa taarifa zao kwenye vituo vya msaada wa sheria.

Hayo yamebainika Jijini Dar es Salaam wakati wa harambee iliyolenga kukusanya fedha kwaajili ya kumalizia ujenzi wa jengo la Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania ambapo mgeni rasmi kwenye harambee hiyo alikuwa Rais mstaafu wa awamu ya Nne Mhe. Dkt.Jakaya Kikwete.

Katika harambee hiyo iliyofanyika katika hoteli ya Dar es Salaam Serena, Rais Kikwete aliipongeza TAWLA kwa hatua kubwa waliyopiga katika kupanua wigo wa shughuli zake nakwamba Chama hicho kumekuwa msaada mkubwa na kimbilio la wanawake wengi hapa nchini wanapopatwa na changamoto kwenye jamii zao hasa kwenye eneo la mirathi.

Amesema kuwa hatua ya TAWLA kujenga jengo la Ofisi zake Jijini Dodoma kunaonesha kukua kwa Chama hicho nakwamba hilo ni jambo la kuungwa mkono.

“Nawapongeza sana TAWLA kwa kutanua wigo wa shughuli zenu Mimi naamini kukamilika kwa jengo lenu Jijini DODOMA kutawanufaisha pia watu wa mikoa ya jirani hasa waishio vijijini” alisema Rais Kikwete.


Aliongeza kuwa katika kipindi cha uongozi wake aliwateua majaji wanawake zaidi ya 30 baada ya kuona jitihada zinazofanywa na TAWLA katika kuwatetea wanawake wanaopitia changamoto mbalimbali katika Jamii.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TAWLA Tike Mwambipile aĺisema kuwa upo mwamko mkubwa wa wanawake kutafuta msaada wa sheria wanapopatwa changamoto mbalimbali katika jamii lakini wanachelewa kufika kwenye vituo vya kupata msaada nakwamba wapo miongini mwao wanaotumia vishoka na hivyo kujikuta wakiharibikiwa kutokana na upotevu wa muda.

“Tanzania tuna sheria nyingi ambazo ni nzuri zinazomlinda na kumsaidia mwanamke hivyo wanawake wakichukua hatua ya kufika kwenye vyombo vya Sheria wanapata msaada wa haraka” Ameeleza.

Ameongeza kuwa Serikali imejitahidi kwa kiasi kikubwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa Sheria nakwamba yapo madawati ya msaada wa sheria kwenye vituo vya polisi ambapo wananchi wanapata huduma za awali kabla ya wao kufikiwa.

Akizungumzia harambee hiyo amemshukuru Rais mstaafu Kikwete kwa kushirikiana nao na kuongoza zoezi hilo na kusaidia kufanikiwa kwa kiasi kikubwa.


“Tunamshukuru sana Rais Kikwete kwa kuongoza zoezi zima la harambee yetu tumeweza kufanikiwa kwa kiasi kikubwa zaidi ya asilimia 60, kwakweli tumefurahi sana” aliongeza.

Harambee hiyo iliilenga kukusanya fedha kiasi cha Shilingi milioni 100 kwaajili ya kumalizia ujenzi wa jengo la TAWLA pamoja na Samani zake ambapo jengo hilo lipo eneo la ilazo Jijini Dodoma.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments