MIAKA 60 YA UHURU: HAKI ZA BINADAMU ZATAKIWA KUWA KIUNGO MUHIMU KATIKA UHURU WA NCHI

 

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Amon Mpanju (kulia) akizungumza jambo na Mratibu Kitaifa wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC ) Onesmo Olengurumwa Kongamano la Tathmini ya hali ya Haki za binadamu ndani ya miaka 60 ambalo limefanyika leo jijini Dar es salaam
Mratibu Kitaifa wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC ) Onesmo Olengurumwa akizungumza katika Kongamano la Tathmini ya hali ya Haki za binadamu ndani ya miaka 60 ambalo limefanyika leo jijini Dar es salaam
Aliyekuwa Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu nchini (LHRC) Dkt Hellen Kijobisimba (kushoto) Mwenyekiti chama cha Siasa nchini cha NCCR Mageuzi James Mbatia (kulia) wakifuatilia kwa makini mjadala katika Kongamano la Tathmini ya hali ya Haki za binadamu ndani ya miaka 60 ambalo limefanyika leo jijini Dar es salaam


Baadhi ya washiriki katika Kongamano la Tathmini ya hali ya Haki za binadamu ndani ya miaka 60 ambalo limefanyika leo jijini Dar es salaam.

......................................

NA MUSSA KHALID,DAR ES SALAAM

Katika kuelekea miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara,Serikali imesema itaendelea kukuza na kuendeleza haki za binadamu katika makundi mbalimbali pamoja kuboresha maendeleo nchini ili watanzania waweze kuzipata haki zao kwa wakati.

Hayo yameelezwa jijini Dar es salaam na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Amon Mpanju wakati akifungua Kongamano la Tathmini ya hali ya Haki za binadamu ndani ya miaka 60 katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambalo limeandaliwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC) pamoja na Wizara ya Katiba na Sheria.

Naibu Katibu Mpanju amesema ni vyema waTanzania wakashirikiana na serikali katika kusimamia haki zao katika kuleta maendeleo nchini kwani jambo kuzilinda haki za binadamu sio la serikali pekee bali ni la watu wote.

‘Ukiangalia toka mwaka 1961 tunapata uhuru viongozi wetu hususani Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliweka misingi iliyozingatia haki za binadamu utaona kauli alizokuja nazo za kupambana na ujinga,umaskini na maradhi ililenga kuhakikisha wananchi wanawezeshwa kiuchumi kwa kupata elimu na huduma za afya’amesema Mpanju

Awali akizungumza Mratibu Kitaifa wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC ) Onesmo Olengurumwa amesema wameamua kuwa sehemu ya miaka 60 ya uhuru hivyo wamefanya tathmini ili kuangalia haki kwani ndio kiungo muhimu katika uhuru wa nchi.

‘Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaendeshwa kwa misingi ya haki na utawala bora hivyo yote yapo katika katiba yetu na tumekuwa tukiyafanyia kazi’amesema Olengurumwa

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora,Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu amesema kuelekea kuadhimisha Dec 10 siku ya haki za binadamu ni vyema ikaendelea kufanywa tahmini ya kuzisimamia haki za binadamu ili kutoka katika changamoto na kusaidia wananchi kupata haki zao.

Amesema katika miaka 60 ya uhuru yapo mambo mbalimbali ambayo yamefanywa na Serikali,Asasi za Kiraia pamoja na wadau wengine wa haki za binadamu na maendeleo hivyo ameeleza kufanywa tathimin kila baada ya miaka itasaidia kuweka mazingira mazuri kwa watanzania.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Siasa nchini cha NCCR Mageuzi James Mbatia amesema suala la haki za binadamu linapaswa kuzungumzwa mara kwa mara ili haki mbalimbali zikiwemo haki ya kusikiliza,Utu wa mwanadamu,haki za kuweza kuishi zikaonyesha mazingatio.

Mdahalo huo umewashirikisha wadau mbalimbali maarufu nchini akiwemo Aliyekuwa Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu nchini (LHRC) Dkt Hellen Kijobisimba,Kaimu Jaji Mkuu wa Zanzibar  na mabalozi kutoka maeneo mbalimbali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments