MKUU WA GEREZA AFUNGWA JELA KWA KUIBA FEDHA ZA MFUNGWA





MAHAKAMA nchini Rwanda imemhukumu kifungo cha miaka mitano jela aliyekuwa mkuu wa gereza kuu la Kigali kwa kuiba fedha kutoka katika akaunti ya mfungwa, raia wa Uingereza.

Innocent Kayumba amehukumiwa kifungo hicho pamoja na aliyekuwa msaidizi wake, Eric Ntakirutimana, lakini wamekata rufaa kupinga hukumu hiyo.

Wawili hao wametiwa hatiani kwa wizi wa zaidi ya TZS milioni 21 kutoka kwenye akaunti ya mfungwa huyo. Wizi uliofanyika kupitia kadi ya benki ambayo uongozi wa gereza ulikuwa unaishikilia.

Viongozi hao walichukua kadi hiyo (Visa Card) baada ya kubaini akaunti ya benki ina fedha ndipo wakamlazimisha mfungwa mwingine ambaye ni mjuzi wa teknolojia ya mawasiliano kuidukua.

Mahakama imemwachia huru mfungwa aliyedukua baada ya kujiridhisha kwamba alilazimishwa kufanya hivyo na viongozi wa gereza.

Kayumba ambaye ni afisa wa jeshi mwandamizi alihamishiwa kwenye mamlaka ya gereza mwaka 2014, akiwa mkuu wa gereza Magharibi mwa nchi hiyo kabla ya kuhamishiwa jijini Kigali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments