DC MBONEKO AZINDUA KAMPENI YA UPANDAJI MITI MANISPAA YA SHINYANGA KUADHIMISHA MIAKA 60 YA UHURU


Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akipanda mti wakati akizindua Kampeni ya Upandaji Miti katika Manispaa ya Shinyanga.


Na Malaki Philipo -Shinyanga

Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga imezindua Kampeni ya upandaji wa miti ya matunda na vivuli kuelekea katika maadhimisho ya miaka 60 ya Uhuru wa Tanganyika, na miaka 59 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwa ni nyenzo moja wapo ya kukabiliana na madhara yanayosababishwa na mabadiliko ya tabia nchi.

Uzinduzi huo umefanyika leo Novemba 20,2021 katika viwanja vya machinjio ya ng’ombe ya Kisasa kata ya Ndembezi ambao umeongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko na kuhudhuriwa na viongozi na wakuu wa taasisi na Idara mbalimbali za serikali na zisizo za kiserikali, wadau wa maendeleo pamoja na wakazi wa manispaa ya Shinyanga, ambapo jumla ya miti 2,000 imepandwa na kugawiwa wakazi wa eneo hilo.

Akizindua kampeni hiyo Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko amewataka wananchi kuacha tabia ya kukata miti na badala yake waitunze ili kupunguza kama si kumaliza madhara yanayosababishwa na mabadiliko ya tabia nchi, mfano kuongezeka kwa joto duniani.


“Tuendelee kuilinda miti tuliyoipanda kipindi cha nyuma, lakini pia tuendelee kupanda miti mipy, tuisimamie iote pamoja na kuhakikisha usalama wa miti ili mifugo isiharibu ili miti iwe imara” amesema Mboneko.


“Na safari hii Shinyanga tuna Kampeni yetu inasema Shinyanga ya miembe na mikwaju, miembe tunajua ni soko kubwa pamoja na mikwaju pia ina soko kubwa, kwa hiyo tutumie fursa hiyo ya utunzaji wa mazingira na kipato wakati mwingine, tuhakikishe tunapoadhimisha miaka 60 ya uhuru tutazame na mazingira yetu”, ameongeza Mboneko.


Mratibu wa Kampeni hiyo Afisa Maendeleo ya Jamii Manispaa ya Shinyanga Octavina Kiwone amesema halmashauri hiyo imeweka malengo ya kupanda idadi ya miti ya matunda na vivuli milioni moja na laki tano, ambapo miti hiyo itagawiwa kwenye taasisi za umma na binafsi, shule za msingi na sekondari.


Kiwone amesema miche mingine ya miti itakabidhiwa kwa pamoja na wakazi wa manispaa ya Shinyanga ili kuunga mkono jitihada za serikali kukabiliana na ongezeko la joto duniani ambalo limesababishwa na mabadiliko ya tabia nchi.


Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Shinyanga Abubakar Mukadam amewataka wakazi wa Shinyanga kushirikiana na serikali katika kutatua changamoto zilizopo kwenye jamii huku akimulika suala la upandaji wa miti na utunzaji wa mazingira.


“Ndugu zangu mnafahamu kila mwaka hali ya hewa inazidi kubadilika ninawaomba kuipa nguvu serikali kwa kushirikiana nayo, kila mmoja kuchukua jukumu la kupanda, kuitunza na kuisimamia miti ili kuleta unafuu wa hali ya hewa nzuri ambayo imeanza kutoweka”, amesema Mukadam.


Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga Jomaary Satura amewashukuru wananchi na wadau mbalimbali waliojitokeza katika upandaji miti huku akibainisha kuwa upandaji miti ni jukumu la kila mmoja katika jamii.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya Upandaji Miti katika Manispaa ya Shinyanga.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya Upandaji Miti katika Manispaa ya Shinyanga.
Mwenyekiti wa CCM Wilya ya Shinyanga Mjini, Abubakar Mukadam akizungumza wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya Upandaji Miti katika Manispaa ya Shinyanga.
Zoezi la upandaji miti likiendelea
Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi Said Pamui akipanda mti wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya Upandaji Miti katika Manispaa ya Shinyanga.
Uzinduzi wa Kampeni ya Upandaji Miti ukiendelea
Wananchi wakiangalia miche ya miti

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments