BENKI YA NBC YATOA MSAADA WA MIFUKO 920 YA SARUJI UJENZI WA MABWENI SHULE YA KIRIBA MUSOMA


Makabidhiano ya saruji yakiendelea

Na Mussa John Mara

Benki ya NBC imetoa mifuko mia 920 ya saruji yenye thamani ya shilingi milioni 21 katika shule ya sekondari Kiriba iliyopo halmashauri ya wilaya ya Musoma Mkoani Mara ili kuunga juhudi za wananchi za ujenzi wa mabweni mawili ya wasichana na wavulana.

Akizungumza wakati wa kukabidhi saruji hiyo Meneja wa NBC Tawi la Musoma Sophia Lyimo alisema lengo la NBC ni kutoa msaada kwa jamii inayowazunguka na ni jambo wamekuwa wakilifanya hivyo kutolewa kwa saruji hiyo ni kuhakikisha wanaunga mkono jitihada za wananchi kwa ajili ya ujenzi wa mabweni katika shule hiyo.

Lyimo alisema kuwa kutokana na changamoto ya wanafunzi wanaosoma katika shule hiyo kutembea umbali mrefu imewalazimu kuungana na serikali ya Mhe. Rais Samia Suluhu iliyotoa kiasi cha shilingi Milioni sitini (60) kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vitatu vya madarasa na wananchi kuamua kujenga mabweni hivyo saruji hiyo itasaidia sehemu flani kufikia kiwango wananchi wanachokihitaji.


“Lengo letu ni kuhakikisha ndoto za watoto hawa zinafikiwa nakumuunga Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan katika utoaji wa elimu bora kwa hiyo tunakabidhi mifuko hii ya saruji kwani furaha ya NBC nikuona watoto wanaondokana na changamoto hasa katika swala la elimu”,alisema Lyimo.

Mkuu wa shule ya Sekondari Kiriba Mtani Shadrack Paul ameipongeza Benki ya NBC kwa namna ilivyoguswa katika kuchangia shule hiyo ambayo pia inatarajia kufungua kidato cha tano na sita mwaka 2022 hivyo kukamilika kwa mabweni hayo itasaidia mabinti ambao wanatembea kilomita zaidi ya 10 kwenda na kurudi shule.

“Hatuwezi kumsahau mbunge wa jimbo hili Profesa Sopeter Muhongo kwa namna ambavyo anatushirikisha kuhakikisha jambo hili linakamilika kama inavyotakiwa binfasi nimefarijika sana kwa msaada huu kutoka NBC bado tunahitaji wadau wengine wajitoe kusaidia kama walivyofanya Benki hii tulituma maandiko na leo wametupokea ni msaada mkubwa ambao unaungana na nguvu za wananchi kufikia malengo zaidi”, Hamisi Magoti Diwani wa kata ya Kiriba.


Aidha baadhi ya viongozi wa vijiji vitatu wanaoshiriki katika ujenzi wa mabweni hayo ikiwemo Bwai Kumsoma ,Bwai Kwitururu pamoja na Kiriba wamesema msaada huo utakuwa chachu kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kuongeza nguvu kazi katika eneo la mradi ambapo wamesema watahakikisha saruji hiyo inasimamiwa na kufanya kazi iliyokusudiwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments