TUME YA TAIFA YA SAYANSI NA TEKNOLOJIA KUTOA TUZO KWA WAANDISHI WA HABARI ZA UTAFITI


Mwezeshaji wa mafunzo Method Rutechura kutoka COSTECH akizungumza na waandishi wa habari


Na Dinna Maningo,Mwanza 

TUME ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) imepanga kuandaa na kutoa tuzo za kushindaniwa kwa waandishi wa habari za utafiti za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu lengo likiwa ni kutoa fursa kwa wananchi kupata taarifa za kisayansi kupitia vyombo vya habari.

Waandishi watakaoshindania tuzo ni wale waliopata mafunzo ya uandishi wa habari za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu yaliyotolewa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia kwa waandishi wa habari kutoka mkoa wa Mwanza,Mara na Kagera yaliyofanyika jijini Mwanza.

Hayo yalielezwa wakati wa mafunzo ya uandishi wa habari za sayansi,teknolojia na ubunifu  na mwezeshaji kutoka COSTECH Method Rutechura alipokuwa akifundisha njia mbalimbali za kusambaza taarifa za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu (STU) kwa watafiti na waandishi wa habari.

Rutechura alisema kuwa lengo la tuzo hizo ni kuleta ushindani kwa waandishi wa habari za kitafiti za Sayansi, Teknolojia na Ubunifu kupitia Magazeti,Redio,TV na Mitandao ya kijamii kwa manufaa ya wananchi ili kuyafahamu mambo mbalimbali ya kisayansi.

"Tume ni mshauri mkuu wa Serikali katika masuala yote yanayohusu Sayansi,Teknolojia na Ubunifu kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi hapa nchini,kabla ya ushauri tume ukusanya,huchakata,husambaza na kuhifadhi taarifa za sayansi,teknolojia na ubunifu kwa watumiaji"alisema 

" Baada ya mafunzo COSTECH itafatilia makala mbalimbali zitakazoandaliwa,kuchapishwa au kurushwa katika vyombo vya habari ,itatoa ruzuku kwa waandishi watakaofanikiwa kuandaa makala na itaandaa na kutoa tuzo za kushindaniwa katika kila kategori"alisema Rutechura.

Rutechura alisema kuwa waandishi waliofanya kazi vizuri COSTECH itawatumia kama mashuhuda katika mafunzo yatakayofuata,itawashirikisha waandishi katika makongamano mbalimbali,itawakaribisha watafiti kuwasilisha matokeo ya tafiti zao kupitia COSTECH TV na itawakaribisha watafiti kuchapicha matokeo ya tafiti zao.

Alisema kuwa Tume hiyo ilitoa mafunzo ya uandishi wa habari za Sayansi, Teknolojia na Ubunifu katika mkoa wa Dar -salaam,Mtwara,Tanga,Dodoma,Unguja na Pemba

Rutechura alisema kuwa baada ya mafunzo ,kwa mikoa hiyo Magazeti yameongoza kuripoti makala nyingi za Sayansi, Teknolojia na Ubunifu ambapo mkoa wa Tanga unaongoza huku YouTube TV Online zikivuta mkia, mkoa wa Unguja ukiwa wa mwisho.

Alieleza kuwa Tanga inaongoza kwa makala 180 kati ya hizo makala za magazeti ni 42,redio 87,TV 27,blog 24,YouTube (Online TV) 0,Tovuti 0,mkoa wa Dar -salaam inajumla ya makala 53 kati ya hizo magazeti ni 34,redio 4,TV 12,Blog 3, YouTube TV Online 0 na Tovuti 0.

Mkoa wa Unguja una makala 41kati ya hizo za magazeti ni 8,Redio 13,TV 16,Blog 4,YouTube TV Online 0,Tovuti 0,Mtwara ni makala 61 makala za gazeti ni 29,Redio 10,TV 14,Blog 8,YouTube 0,Dodoma makala ni 69 za Magazeti ni 25,Redio 18,TV 4,Blog 12,YouTube 1,Tovuti 9,na Pemba ni makala 78 kati ya hizo makala za magazeti ni 14,Redio 16,TV 28,Blog 5,YouTube 3,Tovuti 12.

"COSTECH inatambua aina za vyombo vya habari Redio,Luninga(TV),Magazeti/Majarida mtandao,mitandao ya kijamii (Twitter, Facebook, Instagram, YouTube, WhatsApp, Blogu za Serikali na za Binafsi" alisema Rutechura.

Aliongeza kuwa COSTECH imekuwa ikisambaza taarifa za STU  kwa njia ya maonyesho mbalimbali ya kisayansi,makongamano,warsha,semina,mikutano ya kisayansi,midahalo,na majadiliano ya wazi ya kisayansi,majarida,vijizuhu ,vitabu vya sayansi,vipeperushi,mabango na vyombo vya habari.

Aliwataka waandishi wa habari wa mkoa wa Mwanza,Mara na Kagera waliopata mafunzo kujitahidi kuandika habari za sayansi ili ziwafikie wananchi kwakile alichoeleza kuwa habari za sayansi zinaripotiwa kwa nadra na hivyo kuwakosesha wananchi kupata taarifa za kisayansi kupitia vyombo vya habari.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments