RC MAHENGE ATOA MAAGIZO MAZITO KWA WATENDAJI MANISPAA YA SINGIDA


Viongozi wa Chama na Serikali wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Saatano Mahenge (katikati) wakikagua Stendi ya mabasi Misuna mkoani Singida

Na Edina Malekela, Singida

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Saatano Mahenge amefanya ziara ya kikazi ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo na tathimini ya hali ya uwajibikaji kwa watumishi ndani ya manispaa ya Singida.

Akiwa kwenye Manispaa hiyo Oktoba 18,2021 alibaini kuna uzembe mkubwa unaofanywa na baadhi ya watendaji kwa kuto ekeleza kwa maksudi takwa la kisheria la kuhakikisha wanatenga asilimia kumi ya mapato wanayokusanya kila mwezi kwa ajili ya makundi ya wanawake , vijana na wenye ulemavu.

"Nakuagiza Mkurugenzi kufikia mwezi huu mwishoni nataka fedha zote za asilimia kumi ziwe zimetengwa hata kama mnakusanya mapato kidogo. Hii haimwepeki ukikwepa ni sawa na kuichelewesha na kuilimbikiza ", alisema Mahenge.

Akiwa kwenye Machinjio kuu ya Manispaa hiyo iliyopo katika kata ya Mughanga, baada ya kupokea taarifa za kero mbalimbali zinazotokana na uchakavu wa miundombinu ya machinjio hiyo, Mkuu wa Mkoa aligiza kuhamisha machinjio hiyo na kuipeleka eneo la Ng'aida kata ya Kisaki ili kupisha makazi ya watu.

Machinjio hiyo ambayo huchinja wastani wa ng'ombe 40 na mbuzi 20 kwa siku ilijengwa miaka ya 70 iliyopita kwa sasa imekosa ubora kutokana na kukithiri kwa kasoro mbalimbali zinazotokana na uchakavu wa miundombinu yake ikiwemo kero ya utiririshaji wa maji taka na mbolea kwenye makazi ya watu hasa kipindi cha mvua.

Aidha akiwa Stendi Kuu ya Mabasi ya Abiria Misuna aliagiza kuundwa kwa kamati ndogo ya tathimini ambayo itajumuisha madiwani wasiopungua watatu na wataalamu ili kufanya 'stadi' ya je mapato yanayokusanywa ni halali au la.

"Tengenezeni kikundi cha watu watatu waje washinde hapa muda wote kuanzia asubuhi mbaka jioni kufanya 'analysis ' ya kina na watalamu kubaini chanzo hiki kinaweza kikatoa shilingi ngapi wakati wa 'pick ' na usio 'pick'; "alisema Mahenge".

Hata hivyo badala ya kukusanya takribani Milioni 45 kwenye chanzo hicho bado kumekuwa na hali ya kusuasua kwenye makusanyo kutokana na kile kilichoelezwa na viongozi wa Manispaaa kuwa kuna baadhi ya watumishi wasio waaminifu wanakwamisha jitihada hizo.

Pia Mkuu wa Mkoa alitembelea Maziwa ya asili ya Kindai na Munangi na kuagiza zoezi la kusafisha fukwe pembezoni mwa maziwa hayo yote ikiwemo lile na singidani kuanza mara moja na atarudi kwa ukaguzi ndani ya mwezi mmoja kuanzia sasa.

"Katika vitu ambavyo Mwenyezi Mungu ameijalia Singida ni pamoja na haya Maziwa. Huu ni utajiri na urithi wa pekee sana ili urithi huu tuweze kuufaidi ni lazima tutengeneze mazingira mazuri kwa watalii kuanza kufika na kutazama vivutio hivi,"alisema Mahenge".

Mkuu wa Mkoa wa Singida dkt Binilith Saatano Mahenge  akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Manispaa ya Singida wakati wa ziara yake ya kikazi.
Mkurugenzi wa  Manispaa ya Singida  Zefrin Lubuva  akitoa maelekezo ya namna stendi kuu ya Misuna inavokusanya mapato.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments