MO DEWJI AMCHENJIA CHAMA KISA HAJI MANARA

Staa wa Simba, Clatous Chama jana jioni ameonja joto ya jiwe baada ya kuchenjiwa kibao na muwekezaji wa klabu hiyo, Mo Dewji kisa Haji Manara.


Chama akiwa Live Insta kwenye mkutano wake na mashabiki ambao Mo alikuwemo, aliulizwa swali kuhusu kuondoka kwa Haji Manara ndani ya klabu ya Simba, kwenye kujibu Chama alimsifia Haji kitendo ambacho kilionekana kumchefua Mo.

Mo alimuuliza Chama "Haji ndiye aliyekulipia ada ya uhamisho?" Chama akiwa anamjibu Mo alijibu kwa kuomba msamaha kama amemkwaza, Mo akamuuliza tena Nani aliyekulipa Ada....Haji?  baadae Chama alipotaka kujibu Mo akamwambia anatoka kwenye mkutano huo.


Hat hivyo Chama amenukuliwa akisema "Kama Miquissone akiondoka, mimi pia ikija ofa nzuri klabu ikakubali nitaondoka. Nimekaa Simba miaka mitatu, nimefanya mambo mazuri, mashabiki wajue kuwa haya ni mambo ya kawaida yanatokea. Nilishasema tangu awali kama muda ukifika na mimi nitaondoka endapo ofa itakuja na Simba ikikubali,”.

Chama ambaye amekuwa na mchango mkubwa kwa klabu hiyo tangu ajiunge nayo mwaka 2018, aliongeza: “Ukitazama miaka yangu mitatu hapa Tanzania, nadhani nimefanya vizuri kwa timu, ninauhakika mashabiki wanapaswa kuelewa, endapo kuna klabu kubwa itajitokeza tutakaa na kujadili tukikubaliana na Simba ikikubali nitaondoka.”

Kwa misimu yote mitatu ambayo ameichezea Simba, Chama ameiwezesha klabu hiyo kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu mara tatu, huku ikibeba Kombe la FA mara mbili mfululizo na kufika hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika mara mbili.

Tayari Simba ipo katika mipango ya kuboresha kikosi chake na imeshatangaza usajili wa wachezaji wawili, winga Mmalawi Peter Banda pamoja na mshambuliaji Yusuph Mhilu kutoka Kagera Sugar.

Mtendaji Mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez, alimwambia mwandishi wetu kuwa, bado wataendelea kutangaza usajili mpya kwa ajili ya kukiimarisha kikosi hicho kwa michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika na ile ya ndani. “Kwa sasa kazi yetu ni moja tu, kutangaza usajili, mambo mengine tunayaweka kando kwanza,” alisema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post