MAAFISA BIASHARA WANAOGHUSHI LESENI WAONYWA


Na Dotto Kwilasa, Dodoma

AFISA Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (Brela) Godfrey Nyaisa amewaonya Maafisa biashara nchini  wanaoghushi leseni na kutengeneza vitabu feki kuacha tabia hiyo huku akisisitiza kuwa kitendo hicho kosa kisheria kwani  kinahujumu uchumi.

 Nyaisa  ametoa onyo hilo leo Jijini Dodoma wakati  akifungua mafunzo ya siku tano kwa Maafisa biashara kutoka mikoa ya Morogoro,Singida na Dodoma kuhusu sheria ya leseni za biashara.

Amesema kuna Halmashauri flani (hakuitaja)Afisa biashara wake  alifoji vitabu vya risiti  na mwisho wa siku alikamatwa jambo linaloleta aibu kwa jamii .

"Maendeleo hayataki uongo uongo ,kutokana na kuepukana na mambo kama haya tunataka kuweka mfumo mzuri wa kuchukua vitabu na leseni kwa njia ya mtandao,njia hii itakomesha wizi,"amesema.

Licha ya hayo amewataka kuzingatia majukumu yao na kuepuka kuwa kikwazo kwa wafanya biashara hali itakayoleta mawasiliano mazuri baina yao na kutengeneza mtandao wa maendeleo.

Amesema kuwa Maafisa biashara wanatakiwa kuwa mstari wa mbele kuwatembelea wafanyabiashara katika maeneo yao na kuwapa elimu  ya ulipaji wa kodi.

"Najua kunasheria za biashara lakini wakati mwingine lazima muongozwe na busara ili kuweza kupata matokeo yaliyo chanya,kwani kufunga biashara siyo suluhisho na pia ilishapitwa na wakati"amesema Nyaisa.

Amesema,Serikali haifanyi biashara ila inatoa huduma hivyo kupitia mafunzo hayo anaamini Maafisa biashara watabadilika na watapata fikra mpya ambapo wataenda kutumika katika kuongoza biashara.

"Kuna maafisa biashara wanapiga sana hela,wawekezaji wanakuja lakini mnawapiga urasimu sana wakati nyie ndio mlitakiwa kuwapa ushirikiano mkubwa",alisema.

Alisema mojawapo ya kazi ya Afisa biashara ni kuhakikisha eneo lake lina wafanyabiashara na wanafahamiana ,lakini utakuta wengine hawatafuti wawekezaji na hata wakija bado tena wanawakandamiza.

Pamoja na hayo Mtendaji Mkuu huyo amewataka kuwatembelea na kutoa elimu kwa wafanyabiashara kwasababu wapo ambao wanafanya biashara bila kuwa na leseni kutokana na kuogopa.

"Mfanya biashara asipokuwa na leseni hawezi kuendelea kwani hatoweza kupata mkopo kutoka bank,lakini pia hakuna biashara inayokuwa yenyewe bila mkopo hata kama una mshahara bado haitoshi kuikuza biashara yako bila mkopo",alisema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments