MKE ADAIWA KUMUUA MMEWE KWA KUMPIGA SHOKA KICHWANI


Mfano wa shoka

Na Mwandishi wetu, Babati
MKAZI wa Kijiji cha Garanja, Kata ya Tlawi, Wilayani Mbulu, Mkoani Manyara, Maria Suruhu (56) anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kumuua kwa kumpiga kichwani na shoka mume wake Lego Kerehemi (54).

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Manyara, Kamishna Msaidizi (ACP) Marrison Mwakyoma akizungumza jana amesema tukio hilo limetokea kwenye kata hiyo ya Tlawi.

Kamanda Mwakyoma amesema chanzo cha kifo ni ugomvi wa ndani baada ya mwanamke huyo kuulizwa alipochelewa baada ya wote kutoka kunywa pombe kilabuni.

Amesema mume na mke walienda kilabuni kunywa pombe na walipomaliza waliamua kurudi nyumbani huku wakiongozana wawili barabara.

"Baadaye waliachana njiani kila mmoja akafuata njia yake ila kufika nyumbani mume akawahi kufika na mke akachelewa kidogo," amesema kamanda Mwakyoma.

Amesema mume akamuuliza mkewe kwa nini amechelewa kurudi muda wote huo na ndipo akaanza kumpiga kwa kosa hilo.

"Wakati wakiendelea kupigana mke alichukua shoka na kumpiga nalo kichwani mume wake na kusababisha kifo chake papo hapo," amesema kamanda Mwakyoma.

Amesema mwanamke huyo Suruhu anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za mauaji hayo na anatarakiwa kufikishwa mahakamani pindi uchunguzi ukikamilika.

Mkazi wa eneo hilo, Julius Slaa amesema hivi sasa watoto wa familia hiyo wamepata pigo kubwa kutokana na tukio hilo kwani ni sawa na kuwapoteza wazazi wote wawili.

"Baba amefariki dunia kwa kuuawa na mama ambaye hivi sasa yupo mahabusu kutokana na ulevi wao hatima ya watoto itakuwa mbaya," amesema.

CHANZO - MICHUZI BLOG

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments