MATUMIZI YA NYUNGU RUKSA VITA DHIDI YA UVIKO -19... MAFUTA YA 'TETE' SAFI KWA NYUNGU


Kaimu Katibu Mkuu (Afya) Edward Mbanga akifafanua kuhusu maadhimisho ya siku ya Tiba asili ya Mwafrika yanayotarajiwa kuanza 31 Agosti ,2021
**

Na Dotto Kwilasa, Dodoma.

SERIKALI kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na  Watoto kitengo cha Tiba asili imesema jamii inapaswa kuendelea kutumia Nyungu na Tiba asili nyingine zilizosajiliwa katika mapambano ya kujikinga na ugonjwa wa UVICO-19.

Hatua hii imekuja wakati  ambao zoezi la uchanjaji chanjo ya ugonjwa huo likiwa linaendelea huku wanachi wakitahadharishwa kuendelea kuchukua hatua za kujikinga Kwa kuvaa barakoa,kutumia vitakasa mikono na kuepuka misongamano isiyo ya lazima.

Akiongea mapema leo Agosti 20,2021 Jijini Dodoma wakati akizungumzia maadhimisho ya siku ya Tiba asili ya Mwafrika inayotarajiwa kuanza 31 Agosti,2021 Kaimu Katibu Mkuu (Afya) Edward Mbanga amesema hatua hiyo itasaidia kuboresha afya na kujikinga na magonjwa mbalimbali.

Mbanga amesema, Tanzania ikiwa inajiandaa kuungana na mataifa mengine 47 ya Afrika kuadhimisha siku ya Tiba asili,maadhimisho hayo yataenda sambamba na uelimishaji na maonyesho ya bidhaa za Tiba asili ili kuenzi uendelezaji na uboreshaji wake Katika nchi za Afrika.

Hata hivyo ameishauri jamii kuzingatia Tiba hiyo kwa utaratibu na kuepuka ushauri wa kishirikina kwamba sio tiba ya magonjwa bali ni uchonganishi unaoipaka matope tasnia hiyo na kuwataka Waganga wa namna hiyo kuripotiwa.

Kutokana na hayo Kaimu Katibu Mkuu huyo ametumia nafasi hiyo kuwataka Waganga wa tiba asili  kutumia kanuni ,taratibu na miongozo ya kisayansi  katika kukabiliana na UVICO-19 kwa kuzingatia maelekezo na taratibu za kisayansi.

"Dawa hizi zisiwe mbadala wa chanjo,tuendelee kuchukua tahadhali na hatua muhimu za kujinga kumwomba Mungu kila mmoja kwa imani yake atuponye na kutupa maarifa zaidi ya kuondokana na maradhi,"amesema.

Pamoja na hayo amesema amehimiza Waganga wa Tiba hiyo  kuhifadhi miti dawa  kwenye maeneo mbalimbali
kwa kuzingatia utunzaji wa mazingira.

"Mimea dawa mingi  ni adimu hivyo isipotunzwa inaweza kupotea,Waganga wa tiba asili wana wajibu wa kupanda miti na kuhifadhi kwa kufanya hivi jamii itakuwa na hazina ya dàwa nyingi za tiba asili,"amesema  .

Mbali na hayo amewataka Waganga wa tiba asili kupeleka dawa zao kupimwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali  atakaye thibitisha usalama wa dawa tiba hizo ili ziwe salama.

"Muhimu kutumia dawa hizi kwa kuzingatia wakati uliopo wa kisasa zàidi kwa kupima kwenye maabara ya mkemia Mkuu wa Serikali ili zifanyiwe utafiti kujiridhisha ubora na usalama wake  kuondoa matatizo kwa watumiaji,"amefafanua.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi wa tiba asili (Wizara ya Afya)Dkt.Paul Maame amefafanua kuwa Serikali inaendelea kuboresha tiba asili ili kuendana na wakati .

"Tunapozungumzia Nyungu sio lazima kutumia majani ya miti ,tumeenda kisayansi zaidi, kuna mafuta yanaitwa Tete haya tunashauri kutumia kama nyungu, tumeboreshwa kutoka kujifukiza hadi kuitumia dawa ya kujifukiza iliyotengenezwa kwa mfumo wa mafuta ambapo mtumiaji atatumia tone moja kuchanganya kwenye maji,"amesema.

Naye Katibu wa Kamati ya maandalizi ya maadhimisho ya dawa asili-kitaifa Bonaventure Mwalongo  amesema kuelekea siku ya Tiba asili,Waganga waliosajiliwa wanapaswa kuendelea kufuata sheria,kanuni,miongozo na miiko na kwamba watakaokiuka watachukuliwa sheria za kinidhamu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments