MWIZI ALALA USINGIZI MZITO BAADA YA KUMUIBIA BIBI KIZEE



Kumetokea kisa cha aina yake katika kijiji cha Mutomo, kaunti ya Kitui nchini Kenya baada ya mwizi sugu wa mabavu eneo hilo kuvamia nyumba ya ajuza mmoja na kisha kulemewa na usingizi.

Kwa mujibu wa gazeti la Taifa Leo, Jumatatu, Mei 3,2021 mwizi huyo alishindwa kutoroka baada ya kumuibia ajuza na badala yake alikamatwa na usingizi mzito uliomfanya kutiwa mbaroni.

Mwizi huyo alikuwa na mazoea ya kuwahangaisha wanakijiji huku akivamia makazi yao na kuwashurutusha wampe mali yoyote ya thamani waliyokuwa nayo.

Wakati wa siku ya tukio hilo, jamaa huyo alivunja nyumba ya ajuza akitambua kwamba mwanawe alikuwa amemuachia KSh50,000 za ujenzi. 

Alimshurutisha bikizee huyo atoe pesa hizo huku akianza kufungua radio na televisheni ili aondoke nazo. 

Lakini ama kweli akili ni nywele kila mtu ana zake, ajuza alimuomba mwizi huyo ale kwanza kabla ya kuondoka.

Na kwa sababu alikuwa anakeketwa na njaa, mwizi huyo alikubali kuketi kitako na kuparamia sahani mbili za wali uliokuwa umeandaliwa na bibi kizee kisha aliomba maji akate kiu. 

Badala ya kubebea virago alivyompora ajuza huyo na kuondoka, alivamiwa ghafla na usingizi kisha alilala.

 Akiwa amelala usingizi mzito, polisi waliitwa kwenda kumkamata.

 Alipozinduka kutoka usingizini na kuanza kuwekwa pingu alimwambia ajuza huyo:

 "Kitu gani uliniwekea kwenye chakula? wewe ni nyanya mjanja sana" Bibi kizee naye alimjibu: "Ulinioa mzee. Uzee ni mwili, akili ni ya kijana. Nenda tutakutania kortini".

 Ajuza huyo alisifiwa na wakazi kwa ujasiri wake wakidai mwizi huyo aliwahangaisha kwa muda mrefu.

 Chanzo - Tuko news

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments