GEKUL AONYA WANAOJIHUSISHA UVUVI HARAMU, UKWEPAJI KODI


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul (kushoto) akimsikiliza kwa makini Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Joseph Mkirikiti alipomtembelea ofisini kwake jana.Waziri Gekul yupo mkoani Manyara kwa ziara ya Kikazi.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul (kushoto) akimsikiliza Kaimu Mkurugenzi Msaidizi, Ukuzaji Viumbe Maji, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Imani Kapinga alipokuwa akimpa maelekezo Mwakilishi wa Kampuni ya XIN SI LU,  Suvi Zeng (katikati) alipotembelea eneo la ufugaji wa Samaki katika Mabwawa la Kampuni hiyo jana.
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul (kulia) akipokea samaki aina Sato kutoka kwa Mkurugenzi, Idara ya Uvuvi, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Magese Bulayi alipotembelea  eneo la  Kampuni ya XIN SI LU kutoka China iliyowekeza katika ufugaji wa Samaki kwenye Mabwawa Mkoani Manyara jana.

 

Na Mbaraka Kambona, Manyara

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Pauline Gekul amewataka wale wote wanaojihusisha na uvuvi usiozingatia sheria na taratibu kuacha mara moja kwani Serikali haitakuwa na huruma kwa watakaokamatwa. 

Gekul alitoa onyo hilo alipokuwa akiongea na Wavuvi wa Mkoa wa Manyara alipofanya ziara mkoani humo jana. 

Kwa mujibu wa Waziri Gekul katika operesheni ya kupambana na uvuvi haramu iliyopita ilitumika karibu bilioni 1. 2 jambo ambalo alisema halivumiliki na hivyo aliwataka wavuvi kutoa ushirikiano kwa serikali ili kukomesha vitendo hivyo. 

“Hatutavumilia jambo hili liendelee, Sisi kama Wizara tumesema ni lazima tupate muarobaini wa uvuvi haramu lakini na nyinyi wavuvi muwe tayari kutoa ushirikiano kwa serikali ili uvuvi haramu ukomeshwe mara moja,” alisema Gekul.

Aliongeza kwa kusema kuwa uvuvi haramu ukikomeshwa itasaidia kuokoa mazalia ya samaki na kuongeza idadi ya samaki katika maziwa na maeneo mengine. 

“Kwa kuwa mmeonesha nia ya kutoa ushirikiano katika hili, shirikianeni na viongozi wenu kuanzia leo hizo nyavu haramu zikatupwe, tusisikie tena kuhusu nyavu haramu iwe mwanzo na mwisho ,” aliongeza Gekul. 

Aidha, Waziri Gekul alisema kuwa kipaumbele cha serikali kwa sasa ni kuimarisha ufugaji wa viumbe maji kwa kutumia Vizimba na Mabwawa jambo ambalo anasema likisimamiwa vizuri litaongeza ajira kwa wananchi na kupunguza umasikini na kuchochea uchumi wa taifa letu. 

“Niwaombe Wakurugenzi na Viongozi wengine wa Halmashauri waangalie uwezekano kwenye zile asilimia kumi zinazotolewa na Serikali kwa Vijana, Wanawake na Walemavu badala ya kuwapa mkononi wafanye utafiti ili kujua ujenzi wa mabwawa unagharimu kiasi gani ili wawajengee mabwawa ya kufugia samaki na tukiweza kufanya hivyo tutakuwa tumepunguza tatizo la ajira,” alisisitiza Gekul. 

Katika hatua nyingine, Gekul aliwaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri na Maafisa uvuvi kuwafikia wavuvi wote na kuhakikisha wanalipia leseni za uvuvi ili kuzuia upotevu wa mapato na kukuza pato la Serikali. 

“Hili litekelezwe haraka, kila mtu ajisikie vizuri kulipa kodi ya serikali, lipeni kodi na mpatiwe risiti za mashine za elekroniki kwa kufanya hivyo kutazuia upotevu wa mapato ya serikali,” alifafanua. 

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Babati, Lazaro Twange alisema kuwa maelekezo yote yaliyotolewa na Naibu Waziri wameyapokea na watayafanyia kazi kama ilivyoelekezwa ili sekta ya uvuvi mkoani humo iweze kupiga hatua inayotarajiwa. 

“Tutahakikisha wavuvi wote tunawafikia kwa lengo la kutatua kero zinazowakabili lakini vile vile wale ambao hawana leseni waweze kukata leseni ili serikali iweze kuwatambua na kupata mapato kupitia shughuli za uvuvi,” alisema Twange. 

Mwenyekiti wa Wavuvi, Halmashauri ya Babati, Iddi Hassani alisema kuwa watafanyia kazi maelekezo na watahakikisha wanashirikiana na serikali ili wavuvi wote wawe na leseni za uvuvi na wataendelea kupambana na uvuvi haramu ili kunusuru viumbe maji na kuendelea kufanya uvuvi endelevu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments