MAGUFULI AAPISHWA KUWA RAIS WA TANZANIA ...MITANO TENA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiapishwa na Jaji Mkuu wa Mahakama Kuu ya Tanzania Profesa Ibrahim Hamis Juma kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kipindi cha pili cha Awamu ya Tano leo tarehe 05 Novemba 2020 katika sherehe zilizofanyika katika uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma.
***
Rais Mteule Dk. John Pombe Magufuli ameapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mhula wa pili huku akiapa na kuahidi kuwatendea haki watu wote.

Dk. Magufuli ameapishwa leo Alhamis Novemba 5, 2020 katika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma na Jaji Mkuu Profesa Ibrahim Juma katika tukio lililoshuhudiwa na viongozi mbalimbali wa ndani na nje ya nchi.

Katika kiapo chake , Rais Magufuli ameapa kuitetea, kuilinda na kuhifadhi Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na kuahidi kutumika kwa uaminifu katika kazi zake za Urais.

Baada ya kula kiapo na kusaini hati ya utii alikabidhiwa katiba na mkuki na ngao ambapo pia Makamu wa rais, Samia Suluhu Hassan naye alikula kiapo.

Rais Magufuli ametetea nafasi yake baada ya kushinda kwa kishindo Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 28.10.2020.

Magufuli alishinda kwa kupata kura 12,516,252 ambayo ni asilimia 84 ya kura zote zilizopigwa. Tundu Lissu kutoka chama cha upinzani cha Chadema ameshika nafasi ya pili kwa kupata kura 1,933,271 ya kura zote ziizopigwa.

Jumla ya watu 15,91950 walipiga kura hizo wakati waliojiandikisha kupiga kura walikuwa 29,754,699 kwa mujibu wa Tume ya taifa ya Uchaguzi (NEC).

Hii ni awamu ya pili kwa rais Magufuli kuongoza Tanzania, yeye ndiye alikuwa rais wa tano kuiongoza Tanzania kuanzia mwaka 2015 mpaka 2020 na sasa anatarajia kuongoza mpaka mwaka 2025.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments