POLISI SHINYANGA YAONYA WENYE NIA YA KUVURUGA UCHAGUZI MKUU....RPC ASISITIZA "PIGA KURA ONDOKA KITUONI..KULINDA KURA SIYO JUKUMU LAKO"


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Debora Magiligimba akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Oktoba 26,2020. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Debora Magiligimba akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Oktoba 26,2020

Na Kadama Malunde – Malunde 1 blog

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limesema limejipanga kikamilifu kusimamia zoezi  zima la uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 28,2020 katika hali ya amani na utulivu na kwamba kamwe halitasita kuchukua hatua kali za kisheria kwa mtu au watu au kikundi chochote chenye nia ya kuvuruga zoezi la uchaguzi.

Akizungumza na vyombo vya habari leo Oktoba 26,2020, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Debora Magiligimba amewaomba wananchi wajitokeze kwa wingi kwenda kupiga kura kwenye vituo vya kupigia kura wakiwa na amani bila kuhofia usalama wao.

“Jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga limeimarisha doria za magari na pikipiki,doria za miguu pamoja na doria za mbwa. Lakini pia Askari polisi wa kutosha wamepangwa kwenye vituo vyote vya kupigia kura na maeneo mengine ili kuimarisha ulinzi,hivyo wananchi wote wenye sifa za kupiga kura wajitokeze kwa wingi kwenda kupiga kura kwani amani ipo ya kutosha”,amesema Kamanda Magiligimba.

“Lakini pia niwaombe wananchi mara baada ya kupiga kura warudi nyumbani kuendelea na majukumu yao ya kila siku, wasibakie kwenye maeneo ya kupigia kura. Suala la kulinda kura ni suala la Jeshi la Polisi siyo wananchi”,amesisitiza Kamanda Magiligimba.

Aidha ametoa wito kwa wananchi kufuata sheria,kanuni na taratibu za uchaguzi ili kufanikisha zoezi zima la uchaguzi kumalizika kwa amani na utulivu.

Kamanda huyo wa polisi amewataka wananchi kutoa taarifa mapema za uwepo wa viashiria vya uvunjivu wa amani katika maeneo yao ili viweze kudhibitiwa mapema na kwamba jeshi la polisi halitasita kuchukua hatua kali za kisheria kwa mtu au watu au kikundi chochote chenye nia ya kuvuruga zoezi la uchaguzi.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments