JUKWAA LA WANAWAKE NA VIONGOZI WA KISASA WALAANI BAADHI YA WANASIASA KUTUMIA LUGHA YA VITISHO VYENYE VIASHIRIA VYA UVUNJIFU WA AMANI

Jukwaa la Wanawake na wanasiasa nchini (TWCP/ULINGO) wamelaani tabia za baadhi ya wanasiasa kutumia lugha za vitisho, uvunjifu wa amani na utulivu, katika kipindi cha nngwe ya mwisho ya kampeni za kuelekea uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.

Aidha wameshauri kuchukuliwa hatua kwa baadhi ya vyama vya siasa vinavyofanya siasa za udini kwa kuhusisha viongozi wa dini katika kampeni zao, huku vikitambua kuwa ni kinyume cha Katiba ya nchi na Sheria ya Vyama vya siasa.

Akizungumza kwa njia ya simu wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Wanawake viongozi kutoka vyama mbalimbali vya siasa, Taasisi za kijamii na makundi ya wenye Ulemavu kwa kushirikiana na Jukwaa la Wanawake Wanasiasa (TWCP/ULINGO) Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira na Wenye Ulemavu, Jenista Muhagama, alisema jukumu lililopo kwa wanawake wakati huu ni kuhakikisha amani inadumishwa katika uchaguzi.

Alisema wanawake wanapaswa kuwa mawakala wa amani ili kusaidia Watanzania kuwa na umoja wa kitaifa na kuondokana na mihemko yenye matokeo hasi nchini.

Aliongeza kwa kuwataka wanawake na jamii nyingine nchini, kujitokeza kushiriki kupiga kura kwani ndio wakati sahihi wa kuchagua viongozi watakaokidhi haja na matakwa yao.

Kwa upande wake Mratibu wa Jukwaa hiloambaye pia ni Katibu Mkuu wa Chama cha UDP, Saumu Rashid, alisema kwa umoja wao wanalaani tabia zilizoanza kujitokeza kutoka kwa baadhi ya wanasiasa wakitumia lugha za vitisho na uvunjifu wa amani na utulivu.

“Katika kipindi hiki ambacho tunamalizia kampeni, zimekuwa zikizuka lugha na matamko mbalimbali yanayoashiria uvunjifu wa amani ni vyema tuwe makini,” alisema.

Aidha alishauri kuchukuliwa hatua kwa badhi ya vyama vya siasa vinavyoendeleza siasa za udini kwa kuhusisha viongozi wa dini kwenye mikutano ya kampeni zake, jambo ambalo ni kinyume cha katiba na Sheria ya Vyama vya Siasa.

“Tunavitaka vyama vya siasa kutowatumia viongozi wa dini kwa maslahi yao binafsi ili kutugawa Watanzania hususani katika kipindi hiki cha uchaguzi na baada,” alisema.

Alisema kwa mujibu wa Ibara ya 20(2)(a) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na kifungu cha 9(2)(a) cha sehria ya Vyama vya Siasa sura ya 258, vinakata Chama cha siasa kufanya siasa za udini.

Alipongeza Jeshi la Polisi, kwa namna linavyofanya kazi kwa weledi, uadilifu katika ulinzi wa raia na mali zao hususan kwenye kipindi cha Uchaguzi.

Naye Mjumbe wa Jukwaa hilo ambaye pia ni mwakilishi wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT), Ottow Mgeni, alisema kwa kuwa wanawake ndio wasimamizi wa njamii ni wajibu wao kukemea viashiria vyote vya uvunjifu wa amani nchini.

Alisema wanasiasa wanatakiwa kutambua kuwa mshindi yeyote wa Uchaguzi huo, atatokana na chaguo la wananchi hivyo wasijihusishe katika njama zozote zenye dhamira ya kuhatarisha amani ya nchi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments