AIRO AMNADI MGOMBEA UDIWANI CCM, AELEZA ALIVYOPATA CHANGAMOTO KUCHANGIA MAENDELEO KATA ZA MADIWANI WA UPINZANI


Aliyekuwa mbunge wa jimbo la Rorya Lameck Airo akizungumza na wananchi wa kata ya Nyahongo wakati wa uzinduzi wa kampeni za mgombea Udiwani

Na Dinna Maningo,Rorya.
Aliyekuwa mbunge wa jimbo la Rorya mkoani Mara kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Mara Lameck Airo amewaomba wananchi wa kata ya Nyahongo kuchagua wagombea kutoka (CCM) Rais,Mbunge na Diwani ili kurahisisha utendaji wa kazi.

Airo aliyasema hayo wakati akimuombea kura mgombea udiwani Samson Kagutu,akiwa mgeni rasmi katika uzinduzi huo,kata hiyo kwa awamu iliyopita ya 2015-2020 imeongozwa na Diwani kutoka Chama cha upinzani cha CHADEMA.

Alisema kuwa wakati wa ubunge wake amepata changamoto hususani katika kuchangia maendeleo kwenye kata zinazoongozwa na Madiwani wa upinzani ambapo baadhi yao walikataa kumpa ushirikiano ili kuleta maendeleo kwenye kata zao.

"Diwani aliyekuwepo hapa alikuwa wa upinzani hakuwahi kunialika na Diwani ndiye Rais wa kata anayetakiwa kunialika mimi,siwezi kukurupuka na kuvamia kuja kuongea na wananchi,yeye ndiye anatakiwa kunikaribisha na ndiyo sababu sikuweza kufika kwenye kata hii.

"Hajawahi hata kuniomba mchango wowote wa kimaendeleo kisa tu mimi ni mbunge wa CCM eti nikifanya maendeleo kwenye kata yake nakijenga Chama Cha Mapinduzi CCM, matokeo yake wananchi wanapata shida,wanapinga maendeleo wao wakiamini maendeleo yanaletwa na Serikali pekee", alisema Airo.

Alisema kuwa Madiwani wa upinzani waliompa ushirikiano alichangia maendeleo kwenye kata zao kwa kuwa wakati wa uchaguzi kata hizo za upinzani zilimpatia kura nyingi za Ubunge.

"Kuna kata za upinzani ambazo Madiwani walikuwa na ushirikiano na mimi walipohitaji msaada wangu niliwapatia maana najua kabisa wananchi walinipigia kura nyingi kuliko hata kura zao kwanini niwabague kisa tu wanaongozwa na Madiwani wa Upinzani! nimechangia maendeleo mengi kwa pesa zangu za mfukoni", alisema Airo.

Airo aliwapongeza baadhi ya Madiwani kutoka kata za upinzani ambao walimpa ushirikiano katika ubunge wake na kusema kuwa ushirikiano huo umefanikisha kata zao kupata maendeleo.

"Wananchi naomba mpigie kura Kagutu msirudie kosa mpeni Jafari Chege madiwani wa CCM ili asipate changamoto kuwaongoza,nawapongeza wapinzani kata ya Ikoma Diwani alikuwa wa Chadema lakini amefanya maendeleo makubwa,Ikoma wananchi walijitolea kujenga madarasa 8 wakaniomba mchango wa mabati nikapeleka madarasa yote 8 yakaezekwa wamefanya mengi mazuri hivyo hivyo na kata ya Nyathorogo na kata zingine za upinzani.

" Wapo ambao hawakuonyesha ushirikiano wala hawakutaka msaada wangu, kuna kata ya Goribe iliongozwa na diwani wa upinzani nilipeleka Saruji mifuko 100 ikaganda bila kutumika kisa kwamba nikifanya maendeleo napata sifa lakini wanasahau kwamba unapofanya maendeleo kwa wapinzani na wana CCM wenzangu baadhi wanaona ni kama nawajenga Chadema lakini nawaambia siwezi kuacha kuchangia wananchi walionipigia kura",alisema Airo.

Airo alisema kuwa kata hiyo ilipoongozwa na CCM yalifanyika maendeleo."Alipoongoza Musa tulishirikiana ilikuwa kata kubwa tukapambana ikagawanywa kuwa kata mbili ya Nyahongo na Kinyenche,wanafunzi walikuwa wanatembea umbali mrefu wasichana wanaanza wako 50 wakimaliza hawafiki 10,wengine walibeba ujauzito tukapambana zikajengwa Sekondari na mafanikio mengine",alisema.

Mgombea Udiwani kata hiyo Samson Kagutu aliwaomba wananchi wamchague na kwamba wakimpa kura za kutosha atahakikisha kata hiyo inapata maendeleo.

Katika uzinduzi huo wa kampeni za mgombea Udiwani,baadhi ya wagombea udiwani kutoka kata zingine walimwombea kura na kuahidi kufanya maendeleo kwenye kata zao endapo wakichaguliwa.

Aliyekuwa mbunge wa jimbo la Rorya Lameck Airo akizungumza na wananchi wa kata ya Nyahongo wakati wa uzinduzi wa kampeni za mgombea Udiwani





Kulia ni mgombea Udiwani kupitia CCM kata ya Nyahongo,kushoto ni Lameck Airo aliyekuwa mbunge wa jimbo la Rorya


Watu wenye ulemavu wa viungo wakitoa burudani

Lameck Airo akiburudika na watu wenye ulemavu kata ya Nyahongo



Waliotia nia udiwani kata ya Nyahongo lakini kura hazikutosha wakiwaombea kura wagombea wa CCM

Kikundi cha kwaya kikitoa burudani wakati wa uzinduzi kampeni za Udiwani kata ya Nyahongo








Wananchi kata ya Nyahongo wakiwa kwenye uzinduzi wa kampeni za mgombea udiwani



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post