DR MWINYI AAHIDI NEEMA KWA WAJANE

Mgombea urais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk Hussein Mwinyi, amekutana na Jumuiya ya Wanawake Wajane na kuahidi kuwatambua kwa kuwaingiza katika mfuko wa hifadhi ya jamii na kupata mikopo itakayowasaidia kujikwamua kimaisha na kupata maendeleo ya kiuchumi.


Akizungumza na wanawake hao mjini Unguja jana, Dk Mwinyi alisema akichaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar atayatambua rasmi makundi maalumu ikiwamo walemavu, wazee na wajane na kuwasaidia kuzitumia fursa mbalimbali za kiuchumi.

Alisema katika serikali yake, makundi hayo yatapatiwa mikopo isiyokuwa na riba, ambapo serikali itachukua jukumu la kulipa riba katika taasisi za fedha.

“Nazitambua changamoto kubwa zinazowapata wanawake walioachwa na waume zao na kuishi katika mazingira magumu, nikichaguliwa nitalichukua suala hilo kwa kuyaingiza makundi maalumu katika mfumo wa kupata mikopo isiyokuwa na riba ili kupata fedha kwa ajili ya kufanya miradi midogo na kuondokana na hali ngumu ya maisha,'' alisema.

Mgombea huyo wa urais wa Zanzibar kupitia CCM, alisema akichaguliwa pia anakusudia kuangalia mfumo mzuri wa sheria za kupambana na udhalilishaji wa kijinsia kwa wanawake hasa wanaoachwa na kuachiwa mzigo wa familia ikiwemo watoto.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527